Ninyi mlioonja huruma ya Mungu, waonjesheni wengine huruma hiyo wala msiibinafsishe!
Baba Mtakatifu Francisko amewaongoza waamini kutoka sehemu mbali mbali za dunia kujiandaa
kikamilifu kuadhimisha Jumapili ya nne ya kipindi cha Kwaresima, Jumapili inayojulikana
kuwa ni Jumapili ya furaha, kwa: kufunga na kusali; toba na wongofu wa ndani; kuabudu
Ekaristi Takatifu pamoja na kuungama dhambi zao. Kwaresima ni kipindi cha toba na
wongofu wa ndani unaopaswa kuwa ni endelevu. Hii inatokana na sababu kwamba, hakuna
mwanadamu anayeweza kujidai kwamba, ni mkamilifu, kumbe anajitaji kujipatanisha na
Mungu pamoja na jirani.
Katika mahubiri yake kwenye Kanisa kuu la Mtakatifu
Petro mjini Vatican, Ijumaa jioni, Baba Mtakatifu amewaambia waamini kwamba, kuna
mambo msingi ambayo waamini wanapaswa kuyazingatia katika maisha yao. La kwanza ni
kujitahidi kuwa watu wapya kadiri ya mpango wa Mungu kwa kutambua kwamba, wao ni watoto
wa Mungu, wafuasi wa Kristo na Kanisa wanaopaswa kugeuza mienendo yao kwa kukazia
utu na heshima yao kama binadamu na wala si kwa utajiri alionao mtu!
Waamini
wajitahidi kuyaangalia maisha yao katika mwanga wa neema kwa kutambua kwamba, moyo
wa mwanadamu unaotekeleza mapenzi ya Mungu, utajitahidi kujielekeza katika kufuata
ukweli badala ya kujikita katika majungu; kugawana mali na utajiri na wale ambao hawakubahatika
badala ya kuiba na kujichimbia katika ufisadi; badala ya kuelemewa na chuki na hali
ya kutaka kulipiza kisasi, mwamini ajitahidi kuwa mpole na mnyenyekevu wa moyo, tayari
kusamehe na kusahau; badala ya kuendekeza majungu na umbea unaoharibu sifa njema ya
watu, mwamini ajitahidi kuona mazuri kutoka kwa jirani zake.
Baba Mtakatifu
anawaalika waamini kujikita katika upendo thabiti na udumifu kwani hii ni sehemu ya
maisha ya Mwenyezi Mungu. Upendo unashinda dhambi na una nguvu ya kuweza kuanza tena
upya kwa kusamehe, kama inavyojionesha katika sehemu ya Injili ya Baba Mwenye huruma,
anayeacha daima mlango wazi, akimsubiri Mwana mpotevu ili aweze kurejea tena nyumbani
kwa Baba, ili kushiriki tena huruma na upole wa Mungu, kwani Yeye ni chemchemi ya
upendo na mwaliko wa kupenda kama anavyopenda Yeye.
Baba Mtakatifu Francisko
anasema, ushuhuda wa upendo unaotolewa na Wakristo sehemu mbali mbali unapaswa kuwa
ni kielelezo cha wafuasi aminifu wa Yesu. Upendo una sifa ya kushirikisha wengine
badala ya kujifungia katika ubinafsi. Kwa asili, upendo uko wazi na una tabia ya kujiongeza
zaidi na zaidi. Baba Mtakatifu anawashukuru wote waliohudhuria Ibada hiyo na kwamba,
kwa muda wa masaa ishirini na manne, wataweza kujipatanisha na Mungu pamoja na jirani
zao. Hili ni tukio ambalo limewashirikisha waamini kutoka katika Majimbo na Parokia
mbali mbali duniani.
Hii ni furaha ya kupokea huruma ya Mungu ili kujenga
na kuimarisha urafiki, tayari kujimaga uwanjani kusherehekea zawadi ya maisha mapya.
Baba Mtakatifu anasema, kwa yule anayeonja huruma ya Mungu anachangamotishwa hata
yeye kuwa ni chombo cha huruma kwa maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii.
Waamini wataonja huruma kwa kuwaonjesha wengine huruma, ili hatimaye, kusherehekea
Pasaka ya Bwana kwa furaha kubwa!