Muswada wa ndoa ya wake wengi yachafua hali ya hewa nchini Kenya!
Baraza la Maaskofu Katoliki Kenya limemwandikia barua Rais Uhuru Kenyatta wa Kenya
kumwomba, asikubali kuridhia muswada wa sheria uliopitishwa hivi karibuni na Bunge,
nchini Kenya wa kutaka kuhalalisha ndoa za wake wengi. Barua iliyoandikwa na kutiwa
mkwaju na Kardinali John Njue, Rais wa Baraza la Maaskofu Katoliki Kenya inasema kwamba,
Kanisa limeendelea kuwa mstari wa mbele katika kukuza utu, maadili na nidhamu katika
maisha ya wananchi wengi wa Kenya, hasa kuhusiana na masuala ya ndoa na familia, kwani
huu ni msingi wa umoja, mshikamano na mfungamano wa maisha ya kijamii.
Hii
ni changamoto kwa Serikali kuhakikisha kwamba, inasaidia kuenzi tunu msingi za maisha
ya ndoa na familia, mambo yanayoakisi maadili na utu wema miongoni mwa wananchi wa
Kenya. Muswada wa sheria uliopitishwa na Bunge la Kenya una vipengele ambavyo kimsingi
vinakinzana na: Sheria asilia, Amri za Mungu pamoja na Mafundisho ya Kanisa; mambo
ambayo hayakuzingatiwa kamwe wakati wa mchakato wa kutunga sheria hii mpya ya ndoa.
Kutokana na mapungufu makubwa ya kimaadili na utu wema yanayojitokeza kwenye muswada
huu, Kanisa Katoliki nchini Kenya, linamwomba, Rais Uhuru Kenyatta kutoridhia muswada
huo.
Marekebisho mengine ya sheria ya ndoa ya Mwaka 2013 yanahusu mgawanyo
wa mali ikiwa kama ndoa itavunjika. Hapa kila mtu atagawiwa kadiri ya mchango wake,
jambo ambalo linapingwa vikali na Wabunge wanawake wapatao 69, kati ya wabunge 349
wa Bunge la Kenya.