Mashahidi wa Injili ya Utamaduni wa kukutana na watu!
Baba Mtakatifu Francisko amewapongeza wanachama wa Chama cha Watu wasioona nchini
Italia kwa jitihada zao za kuwashirikisha watu wenye ulemavu katika uhalisia wa maisha,
alipokutana nao, Jumamosi, tarehe 29 Machi 2014, katika mkutano wao wa kitaifa, kwa
kuongozwa na kauli mbiu "Mashahidi wa Injili ya Utamaduni wa Kukutana".
Tema
ya kukutana inaashilia kwanza kabisa kukutana na Yesu Kristo, ili awawezeshe kuwa
kweli ni mashahidi aminifu wa Injili yake, kama alivyofanya yule mwanamke Msamaria,
alipoambaiwa kuhusu undani wa maisha yake, akatimua mbio kwenda mjini kuwaita watu
wengi kumshuhudia Kristo aliyemwelezea kuhusu maisha yake. Kumbe Shahidi wa Injili
ni mtu aliyekutana na Yesu, akamfahamu, akampenda na kusamahewa dhambi zake. Hii ndiyo
dhana ya kukutana inayogusa undani wa maisha ya mtu na kumkirimia furaha na maana
ya maisha. Hapa aliyeguswa na ujumbe huu anawajibika kuwashirikisha wengine.
Baba
Mtakatifu anasema, mfano wa Msamaria mwema unaeleweka zaidi kwani Yesu alipenda kukutana
na wale waliokuwa wanasukumizwa pembezoni mwa Jamii, watu ambao hawakuthaminiwa hata
kidogo na walibezwa na kutwezwa kama "soli ya kiatu". Yesu alikutana na kuzungumza
na wagonjwa pamoja na walemavu na kuwawezesha tena kuona utu na heshima yao kama binadamu.
Huu ndio utamaduni wa kukutana unaoleta mabadiliko ya ndani.
Yesu anarekebisha
mawazo potofu yaliyokuwa yameenea nyakati zake kwamba, ulemavu ni matokeo ya dhambi,
ndiyo maana anamponya kipofu ambaye baadaye anakuwa ni shahidi wa kweli za Kiinjili
zinazofumbatwa katika matendo makuu ya Mungu; yaani: maisha, upendo na huruma. Wakuu
wa makuhani wanashindwa kuona ukuu wa Mungu na hivyo wanamtuhumu Yesu eti ni "mdhambi".
Yule Kipofu aliyeponywa na Yesu anamtetea na hatimaye anaungama imani na hatima ya
maisha ya Yesu, ambaye alifukuzwa kutoka mjini pale. Yule Kipofu alianza maisha mapya
katika Jumuiya inayojisimika katika imani kwa Yesu, kwani alimwonjesha upendo wa kidugu.
Baba
Mtakatifu anasema, ulimwenguni kuna tamaduni kuu mbili: utamaduni wa kukutana na utamaduni
wa kuwatenga wengine kutokana na magonjwa na hali yao ya maisha. Lakini mtu aliyekutana
na Yesu kwa njia ya imani, anao mwono mpana zaidi unaomsukuma kushirikisha imani yake
kwa jirani. Kwa kutambua mapungufu ya kibinadamu na ulemavu ambao mtu anao, inaweza
kuwa ni fursa makini ya ujenzi wa mahusiano ya kidugu ndani ya Kanisa na Jamii.
Baba
Mtakatifu anawashukuru na kuwahimiza kuendea kutembea katika mwanga huu, kwa kumwilisha
karama ya mwanzilishi wa Chama cha Vipofu Italia, Maria Motta, mwanamke wa imani na
moyo wa kitume. Anawaalika wote katika ujumla wao, kutoa nafasi ya kukutana na Yesu,
anayefahamu ukweli wa moyo wa mwanadamu, mwenye uwezo wa kumweka mtu huru pamoja na
kumpatia matumaini mapya ya maisha.