Askofu Godfrey Mdimi Mhogolo wa Kanisa Anglikan, afariki dunia, Afrika ya Kusini
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Jakaya Mrisho Kikwete amemtumia Salamu za
Rambirambi Dkt. Jacob Chimeledya, Mkuu wa Kanisa la Anglikan Tanzania, kuomboleza
kifo cha Askofu Godfrey Mdimi Mhogolo wa Dayosisi ya Kati, Kanisa Anglikani, Dodoma
kilichotokea tarehe 27 Machi, 2014 katika Hospitali ya Mil Park nchini Afrika Kusini
alikokuwa amepelekwa kwa matibabu.
“Nimepokea kwa masikitiko makubwa taarifa
za kifo cha Mtumishi wa Mungu, Askofu Godfrey Mdimi Mhogolo aliyelitumikia Kanisa
lake la Anglikana kwa uaminifu na uadilifu mkubwa, na ambaye mchango wake kwa maisha
ya kiroho ya Waumini wake unajulikana kwa wengi miongoni mwetu”, amesema Rais Kikwete
katika Salamu zake za Rambirambi.
Rais Kikwete amesema kuondoka kwa Askofu
Mhogolo kumeacha pengo kubwa siyo tu kwa Waumini wa Kanisa la Anglikana katika Dayosisi
yake, Dayosisi ya Kati, Dodoma bali pia kwa Waamini wote wengine wa Madhehebu hayo
kote nchini, na kwa kweli wapenda amani wote popote walipo.
“Ni kutokana na
msiba huu mkubwa, ninakutumia wewe Dkt. Jocob Chimeledya, Mkuu wa Kanisa la Anglikana
Tanzania, na Waamini wote wa Kanisa hilo Salamu zangu za Rambirambi kutoka dhati ya
moyo wangu kwa kuondokewa na Mtumishi huyu wa Mungu aliyejitoa kikamilifu kuwatumikia
Waamini wa Kanisa lake”, ameongeza kusema Rais Kikwete na kuongeza, “Kupitia kwako
naomba pia Salamu zangu za Rambirambi na Pole nyingi ziifikie familia ya Marehemu
Askofu Godfrey Mdimi Mhogolo kwa kuondokewa na Kiongozi na mhimili wa familia yao”.
Rais Kikwete ameiomba familia ya Marehemu kuwa na moyo wa uvumilivu na subira
katika kipindi hiki kigumu cha kuondokewa na Mpendwa wao kwa kutambua kuwa yote ni
Mapenzi yake Mola.
“Ninaihakikishia familia ya Marehemu kuwa binafsi niko pamoja
nao katika kuomboleza msiba huu mkubwa kwa kutambua kuwa msiba wao ni wetu sote. Namuomba
Mwenyezi Mungu, Mwingi wa Rehema aipokee na kuilaza Mahala Pema Peponi, Roho ya Marehemu
Askofu Godfrey Mdimi Mhogolo, Amina”, amemalizia kusema Rais Kikwete katika Salamu
zake.