2014-03-28 10:53:45

Sakramenti ya Ekaristi Takatifu mintarafu mafundisho ya Mtakatifu Ambrosi


Padre Raniero Cantalamessa mhubiri wa nyumba ya Kipapa katika tafakari yake ya tatu ya Kipindi cha Kwaresima kwa Baba Mtakatifu Francisko pamoja na wasaidizi wake wa karibu, Ijumaa tarehe 28 Machi 2014, amezungumzia kuhusu Sakramenti ya Ekaristi Takatifu mintarafu mafundisho ya Mtakatifu Ambrosi.

Baba huyu wa imani alifafanua vyema kuhusu mageuzo kwa kusema kwamba, nguvu ya baraka yapita ile ya maumbile, kwani kwa baraka maumbile yenyewe hujikuta yamebadilika. Neno la Kristo lililoweza kuumba kitu kisichokuwapo bila kutumia kitu, lisingeweza kubadili vitu vilivyopo katika vile ambavyo havikuwepo?

Katika tafakari yake, Padre Cantalamessa amezunguzia kuhusu Fumbo la Ekaristi takatifu, Ekaristi Takatifu kama kielelezo na chemchemi ya baraka ya Agano la Kale kati ya Mungu na Waisraeli. Ekaristi Takatifu ni sadaka na zawadi ya Kristo kwa waja wake. Fumbo la Ekaristi takatifu linaunda Kanisa na kwamba, Ekaristi Takatifu ni Kanisa lenyewe, kumbe wale wanaoshiriki Fumbo la Ekaristi Takatifu wanageuzwa na kuwa ni sehemu ya Fumbo la Mwili wa Kristo yaani Kanisa.

Mtakatifu Ambrosi anasema, Ekaristi Takatifu ni Fumbo la Mwili wa Yesu aliyezaliwa na Bikira Maria, akateswa na kufa Msalabani na alipochomwa ubavuni kwa mkuki, ikatoka maji na damu. Mwili wa Kristo unaweza kueleweka katika maana kuu tatu yaani: Mwili wa kweli wa Yesu aliyezaliwa na Bikira Maria; Mwili wa Kristo, yaani Ekaristi Takatifu na Fumbo la Mwili wa Kristo, yaani Kanisa.

Ekaristi Takatifu ni chimbuko la majadiliano ya Kidini na Wayahudi, kwani kwa Wayahudi, Ekaristi inajulikana kama "Beraka" yaani: Sala ya kubariki na kushukuru: kabla na baada ya chakula. Kwa Wakristo Ekaristi Takatifu ni kielelezo cha Mwana Kondoo wa Pasaka na imepewa hadhi ya juu kabisa na Kristo mwenyewe, kama kielelezo cha Agano Jipya na milele linalofungwa kwa Damu yake Azizi. Yesu anasema Ekaristi ni Mwili na Damu yake inayomwagika kwa ajili ya wengi.

Yesu aliweka Sakramenti ya Ekaristi Takatifu, siku ile iliyotangulia kuteswa kwake, yaani Ijumaa kuu. Mazingira, Sala na vitendo vyote vinafanya rejea kwenye Karamu ya Wayahudi. Yesu anatoa maana mpya ya Karamu hii kwa kuanzisha Agano Jipya na la Milele, kama kielelezo cha sadaka ya wokovu kwa binadamu. Ekaristi Takatifu ni kumbu kumbu endelevu ya Sadaka ya Kristo pale Msalabani.

Kwa mageuzo ya mkate na divai hufanyika mabadiliko ya uwamo wote wa mkate katika uwamo wa Mwili wa Kristo na uwamo wote wa divai katika uwamo wa Damu yake Azizi. Jambo la msingi ambalo linapaswa kuzingatiwa hapa ni imani ya mwamini anayepokea Fumbo la Ekaristi Takatifu.

Yesu amejisadaka na kuwapatia wafuasi wake zawadi kubwa ya Mwili na Damu yake Azizi, kama Sakramenti, mwaliko kwa waamini kuwa kweli ni sadaka hai inayopendeza machoni pa Mwenyezi Mungu. Sadaka ya Kristo ni kielelezo cha hali ya juu kabisa cha upendo kwa Baba yake wa mbinguni na kwa mwanadamu na kwamba, mwanadamu anapaswa kujisadaka na anapokubali kwa kusema Amina, anakubali kuwa ni sehemu ya Ekaristi: Fumbo la Mwili wa Kristo, Fumbo la Kanisa.

Padre Cantalamesaa anasema, hapa Ekaristi Takatifu inaunda Kanisa, changamoto kwa waamini wanaoshiriki Fumbo la Ekaristi Takatifu kuwa ni kielelezo cha upendo wa Mungu kwa jirani zao, kwa kujisadaka na kuwasaidia katika hija ya maisha yao hapa duniani. Ni mwaliko wa kudumisha umoja wa Kanisa la Kristo lililoenea sehemu mbali mbali za dunia kwa kukiri uweza na utukufu wa Kristo.







All the contents on this site are copyrighted ©.