2014-03-28 08:35:49

Familia na utunzaji bora wa mazingira


Dhamana ya Familia katika utunzaji bora wa mazingira katika Jamii ndiyo kauli mbiu inayoongoza warsha ya siku moja iliyoandaliwa na Baraza la Kipapa la Familia kwa kushirikiana na Greenaccord itakayofanyika tarehe 29 Machi 2014. Kanisa linatambua dhamana na wajibu wa familia katika kulinda na kutunza mazingira ambayo ni sehemu ya kazi ya uumbaji.

Lengo la warsha hii ni kuibua mbinu mkakati utakaosaidia kuchangia mawazo kwa ajili ya Maadhimisho ya Sinodi maalum ya Maaskofu kwa ajili ya Familia, itakayoadhimishwa mjini Vatican, kuanzia tarehe 5 hadi tarehe 19 Oktoba, 2014. Familia zinapaswa kusaidiwa kujenga utamaduni wa kulinda na kuhifadhi mazingira. Hii ndiyo changamoto kubwa iliyoko mbele ya Jumuiya ya Kimataifa kadiri ya ushauri kutoka kwa wataalam wa masuala ya mazingira.

Mada hii ni changamoto kwa washiriki kufanya rejea katika hati na nyaraka mbali mbali zilizowahi kutolewa na Mama Kanisa kuhusiana na mazingira, mwaliko na changamoto ya kubadili mfumo wa maisha, unaowajibisha familia.Familia hazina budi kuchangia katika mchakato wa ujenzi wa Jamii inayojikita katika utunzaji bora wa mazingira.

Askofu mkuu Vincenzo Paglia atakuwa ni kati ya wawezeshaji wakuu kwenye warsha hii ya siku moja itakayofanyika mjini Vatican pamoja na kuwahusisha viongozi wakuu wa kidini, wachumi, watafiti na wadau mbali mbali wa mazingira.








All the contents on this site are copyrighted ©.