2014-03-27 07:41:12

Siku kuu ya toba, wongofu na upatanisho!


Kama ilivyokuwa kwa Manabii, wito wa Yesu wa toba na wongofu wa ndani haulengi kwanza kazi za nje yaani kuvaa gunia na kujipaka majivu, kufunga na kujitesa, bali wongofu wa moyo unaogusa undani wa mtu mzima. Bila wongofu huu, matendo ya toba hayana nguvu wala ukweli ndani yake. Wongofu wa ndani husukumwa kuonesha ishara zinazoonekana, vitendo vya mwili, na kazi za toba. RealAudioMP3

Toba ya ndani ni kuelekeza upya kabisa maisha yote, ni kurudi na kumwongokea Mwenyezi Mungu kwa moyo wote, kukataa dhambi na nafasi zake; kuchukua maovu, kwa kujiwekea lengo ka kubadili maisha pamoja na kuendelea kutumainia huruma na neema ya Mungu. Wongofu wa ndani hufumbata maumivu na machungu ya wokovu ambayo Mababa wa Kanisa wameita kuwa ni taabu ya roho au toba ya moyo.

Moyo wa mtu ni mzito na mgumu. Inatakiwa Mwenyezi Mungu ampe mtu moyo mpya. Ikumbukwe kwamba, wongofu wa ndani ni kazi ya neema ya Mungu inayoufanya moyo wa mwanadamu uweze kumrudia tena Muumba wake, kwa kugundua ukuu, huruma na mapendo ya Mungu yasiyokuwa na kifani. Mwamini anapaswa kuonesha masikitiko ya dhambi zake, kwa kumwangalia Yesu aliyeteswa, akafa na kufufuka ili kumkomboa mwanadamu kutoka katika lindi la dhambi na mauti. Kwa Damu yake azizi, Yesu amemkomboa mwanadamu na kuukirimia ulimwengu neema ya toba na wongofu wa ndani.

Mama Kanisa amewawekea watoto wake nyakati za toba zinazojikita katika mazoezi ya maisha ya kiroho, liturujia, hija, kujinyima, kufunga na kusali pamoja na kushiriki katika kazi za matendo ya huruma na kimissionari. Kwa kutambua umuhimu wat oba na wongofu wa ndani, Baba Mtakatifu Francisko, ametenga Ijumaa ya tarehe 28 Machi 2014 kuwa ni siku maalum ya toba na wongofu wa ndani, mwaliko wa kuchuchumilia Sakramenti ya Upatanisho, inayomwonjesha mwamini huruma na upendo wa Mungu usiokuwa na kifani.

Hii ni mikakati ya shughuli za kichungaji inayotekelezwa na Baraza la Kipapa la Uinjilishaji Mpya. Baba Mtakatifu Ijumaa, majira ya jioni ataongoza Ibada ya Upatanisho kwenye Kanisa kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican na baadaye atapata fursa ya kuungamisha baadhi ya waamini watakaoshiriki katika Ibada hii na baadaye kutoa ondoleo la dhambi.

Kuanzia majira ya Saa mbili kamili asubuhi, Kanisa la Mtakatifu Agnes, Bikira Maria, Trastevere na Kanisa la Madonda Matakatifu, yataendelea kutumika kwa ajili ya Ibada ya Kuabudu Ekaristi Takatifu kwa muda wa Masaa 24. Hayo yamesemwa na Askofu mkuu Rino Fisichella, Rais wa Baraza la Kipapa la Uinjilishaji Mpya. Ni tukio ambalo litawahusisha vijana ambao kimsingi ni Wainjilishaji wapya kwa kuwakaribisha vijana wenzao, kuingia ndani ya Kanisa, ili kuonja huruma na upendo wa Mungu kwa waja wake. Ndani ya Makanisa haya, watakutana na Mapadre ambao watakuwa tayari kuzungumza nao na hatimaye, kuwaungamisha.

Tukio hili la kihistoria, anasema, Askofu mkuu Fisichella, litahitimishwa kwa Ibada ya Masifu ya kwanza ya Jioni, Jumapili ya Nne ya Kipindi cha Kwaresima, Ibada itakayofanyika kwenye Kanisa la Santo Spirito in Sassia, Jimbo kuu la Roma.








All the contents on this site are copyrighted ©.