2014-03-27 08:38:47

Nchi Takatifu ni kielelezo cha Injili Hai


Yerusalemu ni kisima cha imani na mahali ambapo mwamini anapata nafasi ya kutembea na kukutana na Yesu katika hja ya maisha yake ya hapa duniani, tayari kushiriki katika mchakato wa kujitakasa kwa kugusa maeneo matakatifu. Ni fursa ya kuweza kuyafahamu zaidi Maandiko Matakatifu, tayari kuganga na kuponya utupu wa ndani, kwa kufunikwa na kivuli cha uwepo wa Kristo mwenyewe katika maeneo haya matakatifu.

Ni mwaliko wa kushiriki katika toba na wongofu wa ndani, kwa kugusa maeneo ambayo yalitumiwa na Yesu mwenyewe katika maisha yake ya hadhara hapa duniani na hatimaye, akajisadaka pale Mlimani Kalvari kwa ajili ya kumkomboa mwanadamu kutoka katika lindi la dhambi na mauti.

Ni tafakari ya kina inayotolewa na Kardinali Leonardo Sandri, Mwenyekiti wa Baraza la Kipapa kwa ajili ya Makanisa ya Mashariki, wakati huu Mama Kanisa anapoendelea kuwaandaa waamini na watu wote wenye mapenzi mema hija ya kitume ya Baba Mtakatifu Francisko huko katika Nchi Takatifu. Kaburi takatifu ni kiini cha imani ya Kikristo kwani linamwonesha Kristo aliyeteswa, akafa, akazikwa na kufufuka. Mji wa Bethelehemu ni mahali ambapo binadamu alitangaziwa ujumbe wa amani kwa kuzaliwa kwa Mwana wa Mungu.

Ziwa Galilaya ni mahali penye umaarufu wa pekee kwani hapa Yesu alituliza dhoruma lililokuwa linawayumbisha mitume kiasi cha kuanza kuchungulia kifo, ni mahali ambapo hata leo hii, Yesu anaendelea kutuliza dhoruba katika maisha na utume wa Kanisa. Kapernaumu ni mahali ambapo Yesu alitoa muhtasari wa mafundisho yake makuu yanayofumbatwa katika Heri za Mlimani. Mjini Yerusalemu, Kanisa linakumbuka Siku ile Yesu alipoweka Sakramenti ya Ekaristi Takatifu na Daraja Takatifu, akawaonesha mitume wake upendo unaojikita katika huduma. Hii ni changamoto kwa waamini wote ndani ya Kanisa.

Yerusalemu ni mji ambamo, Mitume walisali pamoja na Bikira Maria hadi pale Roho Mtakatifu alipowashukia, wakatoka vifua mbele kuwatangazia watu wa mataifa, Injili ya Furaha inayobubujika kutoka kwa Yesu Kristo aliyeteswa, akafa na kufufuka kutoka katika wafu! Kumbe, hija katika Nchi Takatifu inasheheni utajiri mkubwa wa maisha ya kiroho, ndiyo maana Mama Kanisa anawachangamotisha watoto wake na watu wote wenye mapenzi mema, kumsindikiza Baba Mtakatifu Francisko kwa njia ya sala na sadaka zao wakati wa hija yake ya kitume katika Nchi Takatifu.

Kardinali Sandri anasema, hija hii pamoja na mambo mengine, inalenga kukoleza moyo na mchakato wa majadiliano ya amani yanayosimikwa katika ukweli, uwazi, kuheshimiana na kuthaminiana, ili kudumisha misingi ya haki, amani, upendo, udugu na mshikamano wa kweli. Ni mwaliko wa kujenga na kudumisha moyo wa upatanisho wa kitaifa, ili kuvuka vikwazo vya woga na wasi wasi na hatimaye, amani na utulivu viweze kutawala tena katika maisha ya wananchi.

Baba Mtakatifu katika hija yake ya kitume, atatembelea Amman, mahali ambako kuna kundi kubwa la wakimbizi na wahamiaji wanaoteseka kutokana na vita inayozidi kupamba moto huko Mashariki ya Kati. Hapa Baba Mtakatifu anapenda kuwaonjesha wote hao upendo na mshikamano kutoka kwa Mama Kanisa kwa maskini na wote wanaokabiliwa na majanga ya maisha.

Ikumbukwe kwamba, hii ni hija ya kitume inayosimikwa katika kukoleza majadiliano ya kiekumene miongoni mwa Wakristo, kwa kufanya kumbu kumbu ya Jubilee ya Miaka 50 tangu Papa Paulo sita alipokutana, akasali na kuzungumza na Patriaki Anathegoras wa Yerusalemu, miaka hamsini iliyopita. Tukio hili linatarajiwa kufanya kwenye Kaburi Takatifu, mahali ambapo pia pamekuwa ni kielelezo cha utengano kati ya Wakristo. Ndiyo maana kauli mbiu ya Hija hii ya Kitume ina mwelekeo wa Kiekumene, ili wote wawe wamoja!

Kardinali Sandri aliyebahatika kufanya kazi karibu sana na Mwenyeheri Yohane Paulo II anasema, kati ya kumbu kumbu ambazo zimebaki moyoni na akilini mwake, ni pale alipokwenda kumtembelea Mwenyeheri Yohane Paulo II alipokuwa amelazwa kwa mara ya pili Hospitalini Gemelli. Alimwona akiwa katika mateso na mahangaiko ya ndani, akamwambia, naomba mnirudishe nyumbani, niko tayari kuungana na Yesu Kristo aliyeteseka, akafa na kufufuka kwa ajili yetu! Mwenyeheri Yohane Paulo II alionesha ujasiri wa ajabu kiasi cha kuwashangaza wale waliokuwepo chumbani humo.







All the contents on this site are copyrighted ©.