2014-03-27 07:46:05

Majadiliano ya kidini yapate chimbuko lake katika uhalisia wa maisha ya watu!


Kardinali Orlando Beltran Quevedo, Askofu mkuu wa Jimbo kuu la Mindanao, lililoko Kusini mwa nchi ya Ufilippini anasema, ataendelea kujielekeza zaidi na zaidi katika mchakato wa majadiliano ya kidini kama njia ya kujenga na kudumisha misingi ya haki, amani na upatanisho wa kitaifa. RealAudioMP3

Kwa miaka mingi Kardinali Quevedo amekuwa akijihusisha na mchakato wa majadiliano ya kidini na amani kati ya Wakristo na Waislam, Kusini mwa Ufilippini. Hivi karibuni alipokuwa anazungumza na Jumuiya ya Wafilippini mjini Roma alisema kwamba, mpasuko na kinzani kati ya Wakristo na Waislam nchini Ufilippini ni matokeo ya watu kutoaminiana ndani ya Jamii na baadhi ya watu kuendekeza habari za uzushi zisizo na mafao wala mashiko kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya wananchi wa Ufilippini: kiroho na kimwili.

Kardinali Quevedo anasema, majadiliano ya kidini kati ya Waislam na Wakristo hayana budi kujikita katika ngazi kuu tatu: yaani: majadiliano ya maisha; majadiliano yanayoshirikisha mang’amuzi na uzoefu wa maisha ya kiroho pamoja na majadiliano yanayojikita katika taalimungu; majadiliano ambayo yanawahusisha wataalam wa masuala kitaalimungu kutoka katika dini hizi mbili.

Majadiliano yanayojikita katika maisha yanawajengea uwezo waamini wa dini hizi mbili kuheshimiana, kuthaminiana na kusaidiana kwa hali na mali, licha ya tofauti zao za kidini, kwani wote wameumbwa kwa sura na mfano wa Mungu. Majadiliano haya yaanzie katika shule na taasisi za malezi kwa watoto na vijana wa kizazi kipya kwa kutambua kwamba, hawa ndio tumaini na jeuri ya taifa. Ni watoto wanaoweza kusoma na kuishi pamoja kwa amani na utulivu kabisa bila ya chokochoko zozote.

Kardinali Quevedo anasema, majadiliano yanayojikita katika mang’amuzi ya maisha ya kiroho yanalenga kushirikishana tunu msingi za maisha ya kidini zinazofumbatwa katika haki, amani, upendo na mshikamano. Juhudi hizi zinaonekana hasa katika huduma kwa maskini na wote wanaosukimizwa pembezoni mwa Jamii. Hizi ni huduma zinazofanywa na taasisi mbali mbali za dini ya Waislam na Wakristo bila upendeleo, lakini wakisukumwa zaidi na upendo kwa Mungu na jirani.

Majadiliano katika misingi ya kitaalimungu inawapatia waamini wa dini hizi mbili kufahamu mafundisho tanzu ya dini hizi kama yanavyofafanuliwa na wataalam wa taalimungu. Kuna mada zinazofanana katika Kitabu Kitukufu cha Koran na Biblia: Kwa mfano: kazi ya uumbaji na utunzaji bora wa mazingira; athari za mabadiliko ya tabianchi pamoja na maisha ambayo ni zawadi kubwa kutoka kwa Mwenyezi Mungu. Hizi ni tema zinazoweza kufafanuliwa vyema na wataalam wa dini hizi mbili.

Kardinali Quevedo anasema, wengi wanaona kuteuliwa kwake na Baba Mtakatifu Francisko kuwa Kardinali ni kitendawili, ambacho anasema, angependa kukitegua. Tangu mwaka 1974, amekuwa mstari wa mbele katika kuibua, kupanga na kutekekeza mikakati ya shughuli za kichungaji kwa Kanisa Barani Asia. Ametamani kuona Kanisa ambalo liko kati ya watu kwa ajili ya kuwahudumia watu katika mahitaji yao msingi: kiroho na kimwili. Kutokana na mchango wake katika maisha na utume wa Kanisa amewahi kuwa ni kati ya Maaskofu waliopigiwa kura nyingi kwenye Maadhimisho ya Sinodi za Maaskofu.

Mwishoni Kardinali Orlando Beltran Quevedo wa Jimbo kuu la Mindanao anasema kwamba, yeye amesomea na kufaulu kupata shahada ya uzamivu katika masuala ya elimu. Haikuwa rahisi kwake, kwani alipokuwa anakaribia kuhitimisha kuandika kazi yake, Mkuu wake wa Shirika alimtaka kurudi haraka Shirikani kwani alikuwa anahitajika kuwa ni Rais wa Chuo Kikuu cha Notre Dame, hapo utii ukashinda kiburi na matamanio ya kibinadamu. Kwa hakika hapa Waswahili wangelisema, “Usione vinaelea, ujue kwamba, vieumbwa”!








All the contents on this site are copyrighted ©.