2014-03-27 15:37:53

Chama cha Legio Maria chatambuliwa rasmi na Kanisa


Baraza la Kipapa la Walei, Alhamisi tarehe 27 Machi 2014 limekabidhi hati ya utambulisho kwa Chama cha Kitume cha Legio Maria kuonesha kwamba kwa sasa kinatambuliwa rasmi ndani ya Kanisa Katoliki. Hati hii imetolewa na Askofu mkuu Joseph Clemens, Katibu mkuu wa Baraza la Kipapa la Walei katika hafla ambayo imehudhuriwa na viongozi wa Kanisa na wakuu wa Chama cha Legio Maria.

Chama cha Legio Maria kilianzishwa kunako mwaka 1921 huko Dublin, Ireland na Kikundi cha waamini kilichokuwa chini ya uongozi na usimamizi wa Bwana Franck Duff, mfanyakazi katika Wizara ya fedha na baadaye akawa ni Katibu muhtasi wa Waziri wa Ulinzi nchini Ireland. Chama hiki kimedumu takribani miaka 93 bila ya kutambuliwa rasmi na Kanisa. Lakini katika kipindi chote hiki, Chama kimeendelea kuwafunda waamini na hatimaye kikaanza kuwa na utambulisho wake maalum ndani ya Kanisa.

Chama cha Legio Maria kinachota utajiri wake kutoka katika tasaufi ya Bikira Maria pamoja na kujiaminisha kwa nguvu ya Roho Mtakatifu, anayewahamasisha wanachama wa Legio Maria kuwa na malengo makini sanjari na kuchuchumilia utakatifu wa mtu binafsi, pamoja na kuendelea kushiriki kikamilifu katika mchakato wa Uinjilishaji Mpya na huduma makini kwa maskini na wanyonge, bila kuwasahau wale waliokengeuka katika imani yao kwa Kristo na Kanisa lake.

Askofu mkuu Joseph Clemens katika hotuba yake wakati wa kukabidhi Haki na katiba ya Chama cha Legio Maria anasema, chama hiki kimekuwa ni alama wazi kutoka kwa Roho Mtakatifu inayoonesha ari na moyo wa kimissionari kati ya waamini walei, wanavyojitahidi kuyatakatifuza malimwengu kwa njia ya maisha ya kawaida katika familia na sehemu mbali mbali za Kazi. Wanachama wa Legio Maria wanajitahidi kumwilisha katika uhalisia wa maisha ule wito wa kuchuchumilia utakatifu waliopewa wakati wa kupokea Sakramenti ya Ubatizo.







All the contents on this site are copyrighted ©.