2014-03-26 08:12:30

Kiburi cha mwanadamu ni kaburi la maisha yake ya kiroho!


Kwaresima ni kipindi cha toba na wongofu wa ndani; ni kipindi cha kusali na kufunga ni wakati muafaka uliokubalika wa kumwilisha imani katika matendo kwa njia ya huduma ya upendo kwa maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii. Wongofu wa ndani ni mchakato wa kuikimbia dhambi na nafasi zake, jambo ambalo limehubiriwa na Mama Kanisa kwa kitambo kikubwa. RealAudioMP3

Kufunga na kusali ni kitendo cha kukimbilia huruma ya Mungu kwa ajili ya maondoleo ya dhambi, ili kuganga madonda ya dhambi yanayoendelea kumwandama mwamini katika hija ya maisha yake hapa duniani. Kufunga na kusali kunapania kuimarisha utashi na malengo ya mwamini katika kuchuchumilia utakatifu wa maisha kwa kuondokana na na kiburi ambalo limekuwa ni kaburi la maisha ya kiroho.

Hizi ndizo changamoto zinazotolewa na Patriaki Fouad Twal wa Yerusalemu katika ujumbe wake wa Kwaresima kwa Mwaka 2014. Anasema, upendo kwa jirani wanaoteseka kutokana na hali mbali mbali za maisha, hauna budi kuwa ni kielelezo cha umwilishaji wa Injili katika huduma na matendo adili. Huduma hii inapaswa pia kujikita katika mchakato wa upatanisho kati ya Mungu na jirani na kati ya mtu na mtu pamoja na kuonesha jitihada za kupokea huruma na upendo wa Mungu kwa njia ya Sakramenti ya Upatanisho.

Patriaki Twal anasema, sadaka iwe ni kile ambacho mtu katika undani wa maisha yake anakipenda na anapokitoa kinagusa undani wake. Hii ndiyo maana ya matendo ya huruma yanayotekelezwa na waamini katika kipindi hiki cha Kwaresima, kama alivyofanya yule mwanamke mjane aliyetoa hadi senti yake ya mwisho.
Sala ni kati ya mambo msingi yanayotiliwa mkazo na Mama Kanisa katika kipindi hiki cha Kwaresima kwani ni daraja kati ya kufunga na kutoa sadaka. Huu ni mwaliko kwa waamini kuhakikisha kwamba, wanashiriki katika adhimisho la Fumbo la Ekaristi Takatifu, kila Jumapili.

Familia zijenge na kuimarisha utamaduni wa kusali pamoja katika hali ya utulivu bila kuingiliwa na milio ya simu, televisheni au radio, ili kuwawezesha wanafamilia kuindia katika undani wa maisha yao ili wapate kukutana na Yes una hatimaye kumkaribisha ili aweze kuibariki familia inayokutana katika sala.

Patriaki Fouad Twal wa Yerusalemu anawaalika waamini na watu wote wenye mapenzi mema, kujitokeza kwa wingi katika maadhimisho ya Jumapili ya Matawi, Kanisa linapofanya kumbu kumbu endelevu ya Siku ile Yesu alipoingia Yerusalemu kwa shangwe, huku Watoto wa Wayahudi wakitandaza nguo zao njiani, kuonesha ukuu na utukufu wa Yesu Kristo, Masiha na Mkombozi wa dunia. Maandamano ya Jumapili ya Matawi yataanzia kwenye Mlima wa Mizeituni, tayari kuelekea mjini Yerusalemu, ili kushiriki kikamilifu katika Fumbo la Pasaka, yaani: mateso, kifo na ufufuko wa Yesu.

Waamini wanaweza kuboresha hija ya maisha yao wakati huu wa Kwaresima kwa kutembelea na kuangalia Onesho la Picha za Papa Paulo VI alipotembelea Nchi Takatifu yapata miaka hamsini iliyopita.

Ujumbe huu umehaririwa na
Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.








All the contents on this site are copyrighted ©.