2014-03-26 10:27:44

Jamani Mapadre, furahieni Upadre wenu!


Askofu mkuu Josephat Louis Lebulu wa Jimbo kuu la Arusha Tanzania, katika mahojiano maalum na Radio Vatican kuhusu maisha na wito wa Kipadre, wakati huu Baba Mtakatifu Francisko anapotafakari kuhusu Sakramenti ya Daraja Takatifu. Anasema, katika maisha yake, alitamani sana kuwa na elimu bora ya yenye kiwango cha juu, hamu ambayo inapaswa kuratibiwa miongoni mwa Majandokasisi. RealAudioMP3

Alibahatika kuona mifano ya Mapadre wema, watakatifu na wachapakazi hodari, waliomsaidia katika majiundo yake katika maisha na wito wa Kipadre bila kusahau maadhimisho ya Mafumbo mbali mbali ya Kanisa kwa ajili ya kumtukuza Mwenyezi Mungu na mwanadamu kutakatifuzwa. Anasema, Mapadre wanapaswa kuwa na msimamo thabiti katika maisha yao na kwamba, katika hija ya maisha yake ya Kipadre amebahatika pia kukutana na kufanya kazi na waamini walei, waliomsaidia na kumsindikiza katika sala na sadaka zao.

Askofu mkuu Lebulu anasema, furaha ya Upadre ni kuishi na wengine katika Jumuiya, kushikamana katika utume, kwani maisha ya Padre mpweke, yanaweza kumtumbukiza katika majanga na hatimaye, akamezwa na malimwengu. Maisha na wito wa Kipadre unakuwa na kuboreka kwa kujenga na kuimarisha mahusiano thabiti na wengine; kwa njia ya sala na tafakari ya Neno la Mungi; kwa kuwa na msimamo thabiti katika maisha, bila kuyumbishwa yumbishwa kama "Daladala" iliyokatika usukani! Kamwe katika maisha yake hajawahi kujuta kwa nini aliamua kuwa Padre!







All the contents on this site are copyrighted ©.