2014-03-24 10:08:31

Siku ya Mashahidi Wamissionari Duniani


Kunako Mwaka 1993 Kanisa lilianzisha Siku ya Mashahidi Wamissionari Duniani, kama sehemu ya mchakato wa Kumbu kumbu endelevu ya mauaji ya Askofu mkuu Oscar A. Romero wa Jimbo kuu la San Salvador, yaliyotokea kunako tarehe 24 Machi 1980. Tangu wakati huo, kila mwaka ifikapo tarehe 24 Machi, Kanisa lina sali na kufunga kwa ajili ya kuwakumbuka na kuwaombea Wamissionari wote walioyamimina maisha yao kwa ajili ya kutangaza Habari Njema ya Wokovu sehemu mbali mbali za dunia.

Kauli mbiu inayoongoza maadhimisho ya Sku ya XXII kwa Mwaka huu ni “Ushuhuda”, kigezo msingi kwa kila mfuasi wa Kristo kadiri ya maisha na utume wake ndani ya Kanisa. Waamini wanachangamotishwa kuendele kuwa ni mashahidi amini wa Kristo hata katika nyakati hizi za utandawazi na maendeleo ya sayansi na teknolojia. Washuhudie jeuri ya imani yao baada ya kukutana na Kristo Mfufuka anayewapatia hamasa ya kusonga mbele kwa ari na moyo mkuu licha ya madhulumu na nyanyaso wanazokabiliana nazo katika hija ya maisha yao hapa duniani.

Kamwe waamini hawapaswi kukata tamaa hata pale wanaposhindwa kueleweka wakati wa mchakato wa Uinjilishaji Mpya. Kunako Mwaka 2013, Shirika la Habari za Kimissionari, Fides linasema kwamba, kuna Mapadre 20, mtawa mmoja na waamini walei wawili waliouwawa kutokana na imani yao kwa Kristo na Kanisa lake. Wamissionari hawa walioyamimina maisha yao kwa ajili ya Injili wanapaswa kukumbukwa ili kukoleza ari na moyo kwa Wakristo kutoka kimasomaso kutangaza Injili ya Kristo pasi na woga; kwa kusimama kidete kulinda na kutetea haki msingi za binadamu, uhuru wa kuabudu, utu na heshima ya binadamu.

Mchango uliokusanywa katika mkesha wa Siku ya Mashahidi wamissionari Duniani, itasaidia kugharimia miradi ya kimissionari nchini Tanzania hasa katika mikakati ya majiundo makini kwa Majandokasisi nchini Tanzania.








All the contents on this site are copyrighted ©.