2014-03-24 09:57:51

Shemasi Marko Mapinduzi Mwasatila Simbeye


Shemasi ni mhudumu wa Neno la Mungu, msaidizi mkuu katika huduma Altareni na katika kumwilisha matendo ya huruma yanayotekelezwa na Mama Kanisa kwa ajili ya maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii. Ushemasi ni kielelezo cha upendo wa Mungu, unaomkirimia mwamini kuingia na kuishi katika huduma, kama alivyofanya Yesu mwenyewe kwa kumwilisha upendo na huruma ya Mungu kwa binadamu.

Ni sehemu ya mahubiri yaliyotolewa na Askofu msaidizi Paolo Selvadagi wa Jimbo kuu la Roma, wakati wa Ibada ya Misa Takatifu kwa ajili ya kumpatia Daraja la Ushemasi wa mpito Frt. Marko Mapinduzi Mwasatila Simbeye wa Shirika la Wamissionari wa Consolata, Ibada iliyofanyika kwenye Parokia ya Msalaba Mtakatifu, Jimbo Kuu la Roma, Jumamosi, tarehe 22 Machi 2014.

Askofu msaidizi Selvadagi anasema kuna furaha kubwa kwa Mama Kanisa kupata mhudumu kwa ajili ya Kanisa na Ulimwengu katika ujumla wake. Hiki ni kielelezo cha upendo wa Mungu kwa waja wake; upendo unaojionesha katika Maadhimisho ya Liturujia ya Kanisa, Mwenyezi Mungu anapotukuzwa na mwanadamu kutakatifuzwa. Shemasi mpya atakuwa ni mhudumu wakati wa maadhimisho ya Fumbo la Ekaristi Takatifu.

Shemasi amepewa dhamana ya kuwaonjesha watu huruma na ukarimu wa Mungu kwa njia ya matendo ya huruma. Anatumwa kuwatangaza na kushuhudia Neno la Mungu kwa njia ya maisha adili, manyofu na matakatifu. Anapaswa kuwa makini kuwafafanulia watu yale yaliyojiri katika Neno la Mungu na kwamba, Shemasi kimsingi ni mhudumu wa maskini mas wanyonge katika Jamii, watu ambao wanapata upendeleo wa pekee katika maisha na utume wa Kanisa. Shemasi katika hija ya maisha yake, anapaswa kumwilisha mashauri ya Kiinjili.

Shemasi Simbeye amepewa vifaa vya Ibada: mavazi ya ushemasi, Neno la Mungu na Kalisi. Mara baada ya Misa Takatifu amewashukuru wote waliomwezesha kufikia hatua hii na amewakumbuka wazazi na walezi wake ambao wako Jimbo Katoliki la Mbeya, Tanzania. Ibada ya Misa takatifu imehudhuriwa na umati mkubwa wa Familia ya Mungu kutoka Afrika Mashariki.








All the contents on this site are copyrighted ©.