Punguzeni gharama za uchimbaji wa visima ili watanzania wengi wafaidi huduma ya maji
safi na salama!
Waziri mkuu wa Tanzania Mizengo Pinda ameitaka Wizara ya Maji itafute njia mbadala
zitazosaidia kupunguza gharama za kuchimba visima ili wananchi waweze kupata maji
safi na salama. “Wizara ya Maji angalieni uwezekano wa kupunguza gharama za uchimbaji
wa visima ili wananchi waweze kumudu kuchimba visima na wapate uhakika wa maji safi
na salama,” alisema.
Waziri Mkuu ametoa kauli hiyo Jumamosi, Machi 23, 2014,
wakati akifunga Maadhimisho ya Wiki ya Maji Kitaifa yaliyofanyika kwenye Uwanja wa
Jamhuri mkoani Dodoma. “Hivi sasa nimeambiwa gharama ya kuchimba kisima mita moja
ni sh. 150,000/. Je kama mtu anataka kuchimba kisima chenye urefu wa mita 180 au 200
itakuwaje? Ni dhahiri kuwa watu hawataweza kumudu hizo gharama. Angalieni namna ya
kuzipunguza,” alisisitiza.
Waziri Mkuu ambaye alikuwa akifunga maadhimisho
hayo kwa niaba ya Rais Jakaya Kikwete aliwataka wakazi wa mkoa wa Dodoma waendelee
kuthamini dhana ya uchangiaji ili waweze kumudu kuendeleza miradi hiyo. Aliwataka
pia watunze vyanzo vya maji na kutunza miundombinu pamoja na mitambo iliyonunuliwa
kuendesha visima mbalimbali kwani maji yana gharama. “Ninawasihi sana muitunze mitambo
iliyowekwa kuendeshea visima hivi kwani ni vifaa vya gharama sana,” aliongeza.
Mapema,
Waziri Mkuu alizindua kisima cha maji kwenye kijiji cha Mkonze nje kidogo ya mji wa
Dodoma ambacho ujenzi wake umegharimu sh. milioni 519.6/-. Kisima hicho chenye vichoteo
15, kitawanufaisha wakazi 5,887 kati ya 6,869 sawa na asilimia 85.7 ya wakazi wa kijiji
hicho.
“Kabla ya kujengwa kisima hiki, ndoo ya maji ya lita 20 ilikuwa ikiuzwa
sh. 500/- lakini sasa ndoo moja inauzwa kwa sh. 100/- tu,” alisema Mhandisi Mohammed
Kali wakati akitoa taarifa ya mradi huo kwa Waziri Mkuu.
Waziri Mkuu pia aliweka
jiwe la msingi kwenye tenki la maji katika Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOM) lenye uwezo
wa kuhifadhi mita za ujazo 4,500. Ujenzi wake unatarajiwa kukamilika Novemba, 2014.
Akizungumza
na wanajumuiya ya UDOM walioshiriki uzinduzi huo, Waziri Mkuu alisema mradi huo mkubwa
unaenda sambamba na ujenzi wa mradi mwingine mkubwa wa maji taka (recycling plant).
“Ninawasihi muangalie uwezekano wa kutumia maji machafu yatakayosafishwa ili yatumike
kumwagilia miti na maua muweze kutunza mandhari ya UDOM,” alisema.
Akizungumza
katika hafla ya uzinduzi wa tenki hilo, Waziri wa Maji, Prof. Jumanne Maghembe alisema
hadi kukamilika kwake, mradi huo utagharimu sh. bilioni 28. Alisema mradi huo unaojumuisha
ujenzi wa miundombinu ya maji safi na maji taka katika Chuo hicho, umefanyika chini
ya Mpango wa Kuendeleza Sekta ya Maji nchini (WSDP).
Naye Mkurugenzi Mkazi
wa Benki ya Dunia anayesimamia nchi za Tanzania, Burundi na Uganda, Bw. Phillippe
Dongier alisema wao kama wadau wa maendeleo, wanaona fahari kushirikiana na Wizara
ya Maji katika kuleta maendeleo ya sekta hiyo kwa Watanzania.
Uzinduzi wa miradi
hiyo ya maji ni sehemu ya miradi 13 iliyopangwa kuzinduliwa mkoani Dodoma kwenye maadhimisho
ya maji ya mwaka huu. Hata hivyo, mkoa huo una miradi 69 ya maji ambayo ujenzi wake
unaendelea kwa awamu tofauti.