2014-03-24 11:25:36

Papa aunda Tume ya kusimamia ulinzi wa watoto wadogo dhidi ya nyanyaso za kijinsia


Baba Mtakatifu Francisko ameanzisha Tume ya Kipapa kwa ajili ya ulinzi kwa watoto wadogo dhidi ya nyanyaso za kijinsia kama ilivyokuwa imekwisha tangazwa kunako tarehe 5 Desemba 2013. Tume hii inaundwa na Makleri pamoja na waamini walei, baadaye itaongezewa nguvu na wajumbe kutoka sehemu mbali mbali za dunia. Lengo ni kuandaa katiba, mwongozo na shughuli za tume hii.

Akizungumzia kuhusu tume hii, Padre Federico Lombardi, msemaji mkuu wa Vatican anabainisha kwamba, Tume hii itakuwa ni msaada mkubwa kwa Baba Mtakatifu Francisko katika utekelezaji wa utume wake kwa kuhakikisha kwamba, watoto na vijana wanaishi katika mazingira yenye usalama, amani na utulivu kwa ajili ya makuzi na majiundo yao kiroho na kimwili. Tume hii inaundwa na wanawake wanne, ambao wamekuwa mstari wa mbele katika harakati za kutetea utu na heshima ya watoto wadogo dhidi ya nyanyaso za kijinsia.

Tume ya Kipapa ni mwendelezo wa utekelezaji wa mikakati iliyoanzishwa na watangulizi wake katika kulinda watoto na vijana dhidi ya nyanyaso za kijinsia ambazo zilijitokeza katika miaka ya hivi karibuni na hivyo kuchafua utume na maisha ya Kanisa. Huu pia ni utekelezaji wa ushauri uliotolewa na viongozi wa Kanisa na wataalam katika masuala ya malezi na makuzi ya watoto.







All the contents on this site are copyrighted ©.