2014-03-24 08:09:36

Fumbo la Msalaba katika maisha ya kifamilia!


Mpendwa msikilizaji wa Radio Vatican, tujumuike pamoja katika kipindi chetu cha Kanisa la nyumbani. Tukiwa ndani ya kipindi cha Kwaresma, leo tunataka kutafakari juu ya Fumbo la Msalaba wa Kristo. RealAudioMP3

Mama Kanisa katika mafundisho yake, kwa mwanga wa Injili daima ametualika sote, kuyapatanisha maisha yetu na Fumbo la Msalaba wa Kristo. Msingi wa fundisho hili ni mwito wa Bwana mwenyewe anaposema “Mtu ye yote akitaka kunifuata, ni lazima ajikane mwenyewe, auchukue Msalaba wake, anifuate” Mk. 8:34. Kipindi cha kwaresma tunatafakari safari nzima ya Ukombozi ya Kristo, na tunataka kuona ni namna gani sisi, kila mmoja wetu kwa nafsi yake ameuitikia mwito wa kuuchukua msalaba wa maisha na kumfuasa Kristo.

Kuuchukua msalaba wa Kristo na kumfuata maana yake nini? Kuuchukua msalaba haimaanishi tu kuyaambata maisha yetu ya mateso na matatizo ya kila siku. Njia ya msalaba ni safari ya nzima ya Ukombozi ya Kristo. Safari hiyo ya ukombozi ni jumla ya mambo yote ambayo Bwana Yesu aliyafanya, ili kumuunganisha Mwanadamu na Mungu. Yesu alifanya mengi ili kutukomboa, hakuteseka tu (alifundisha, alihubiri, aliwalisha watu, aliwapa matumaini, alikemea maovu, alisali, aliponya wagonjwa, na mwisho akahitimisha hayo yote kwa kujisadaka yeye mwenyewe. Alifanya hayo yote ili kutuunganisha sisi wanadamu na Muumba wetu, ambaye tulimwasi kwa dhambi zetu.

Hivyo, Msalaba ni jumla ya mambo yote ambayo yanatuunganisha na Mungu. Msalaba ni ile kalisi ya wokovu inayotajwa na mzaburi katika zaburi ya 116. Mwaliko wa Yesu kuuchukua msalaba, ni kuwa tayari kukipokea kikombe hicho cha wokovu kila siku, na kuliitia jina la Bwana, yaani kumweka Mungu katika maisha yetu ya kila siku, kuonja uwepo wake na kutegemea wema, msaada na huruma yake daima.

Kuuchukua Msalaba na kumfuasa Yesu maana yake ni kuishi kama alivyotufundisha Yesu mwalimu na kiongozi wetu. Ni kuwa pamoja naye daima. Kama twafurahi tufurahi katika Bwana, kama twateseka, tuteseke pamoja naye, kama tukifa na tufe katika Bwana. Kuuchukua msalaba wetu na kumfuasa, ni mwaliko wa kusali kama alivyosali yeye, kupenda kama alivyopenda yeye, kufariji kama alivyofariji yeye, kuvumilia kama alivyovumilia yeye, na mwisho wa yote tuwe sadaka kwa wokovu wa wengine kama alivyo yeye mwenyewe. Ili kutekeleza vema wito na wajibu huo, tunahitaji imani thabiti.

Mpendwa msikilizaji, kila mmoja katika maisha yake ya kila siku anacho kikombe chake cha wokovu, anao msalaba wake. Kikombe changu cha wokovu na msalaba wangu ni tofauti kabisa na wa kwako. Katika kikombe chako cha wokovu, kuna nyakati za heri zenye mambo mema, kuna nyakati za uchungu na mateso, kuna nyakati za kukata tamaa, kuna nyakati za kujisikia mpweke kiroho na kijamii nk. Kikombe hicho cha wokovu kinajidhihirisha katika nyakati zetu kihistoria kadiri ya uradhi wa Mungu mwenyewe. Analotualika Yesu kufanya hapa, kwanza ni kutambua kuwa tunabeba dhamana ya Ukombozi.

Kila mmoja katika kipindi hiki cha kwaresma, analenga kujipatanisha na kujiambatanisha na Yesu, ili jinsi Yesu alivyo faraja kwa wenye shida, sisi na tuwe hivyo; jinsi Yesu alivyo mwalimu wa ukweli kwa watu, na sisi tuwe hivyo kwa wote wanaopotoshwa na yule mwangamizi wa ulimwengu huu! Jinsi Yesu alivyokuwa huruma na msamaha kwa wakosefu, sisi nasi tuwasamehe na kuwahurumia wakosefu!

Jinsi Yesu alivyo tumaini la waliojikatia tamaa, sisi nasi tuwafumbue macho waliofunikwa na giza la udanganyifu wa ulimwengu huu. Kuuchukua msalaba ni mwito wa kuwa karibu zaidi na Mungu na kuwa karibu zaidi na mwanadamu mwenzetu ili tusaidiane, tuimarishane na tusindikizane katika safari yetu ya kuupanda mlima wa Bwana na kuketi patakatifuni pake.

Katika Kanisa letu la nyumbani, yaani katika familia zetu ambayo kweli ni shule ya fadhila mbalimbali, ni jukumu letu sote kama wanafamilia, kusaidiana, kuinuana, kushikana mkono katika safari yetu ya kiroho, ili kila mmoja aonje upendo na faraja katika familia. Ni katika familia mwanadamu anafundishwa kuwa jirani na mwanadamu Mwenzake. Ni katika familia mwanadamu anafundishwa kuonja na kushiriki upendo, furaha, huzuni na sikitiko la mwanadamu mwenzake. Hatuwezi kuwa wakombozi kwa wenzetu endapo hatuonji shida na maumivu yao au hatuonji uwepo wao katika maisha yetu. Ni katika familia tunajifunza kuvaa maisha ya mwanafamilia mwenzetu.

Ni katika familia mwanadamu anafundishwa kuwa ubinafsi na kujipendelea ni dhambi. Tunaomba na kusihi sana, humo katika familia, watu wafundishwe thamani ya Msalaba na hivyo wawe tayari kuwasaidia wote wenye kulemewa na mizigo mizito ya maisha. Tuyapatanishe maisha yetu na Fumbo la Msalaba wa Kristo, Msalaba ni njia ya kuupandia mlima wa Bwana.
Kutoka Studio za Radio Vatican, ni mimi Padre Pambo Martin Mkorwe OSB.








All the contents on this site are copyrighted ©.