Uchaguzi wa Jumuiya ya Ulaya, usaidie kujenga na kuimarisha mshikamano wa upendo na
udugu
Shirikisho la Mabaraza ya Maaskofu Jumuiya ya Ulaya, COMECE, linawaalika waamini na
wananchi katika ujumla wao kuhakikisha kwamba, wanajikita katika kujenga na kuimarisha
umoja na mshikamano, wakati wa uchaguzi mkuu wa Jumuiya ya Ulaya, unaotarajiwa kufanyika
kati ya tarehe 22 hadi tarehe 25 Mei, 2014. Kardinali Reinhard Marx, Rais wa COMECE
anabainisha kuhusu athari za myumbo wa uchumi kimataifa, lakini zisiwe ni kikwazo
katika ujenzi wa utamaduni wa mshikamano wa upendo miongoni mwa Jumuiya ya Kimataifa.
Maaskofu
katika mkutano wao, wanawataka wananchi wa Jumuiya ya Ulaya kuwa makini na viongozi
watakaowachagua kuongoza kwa kipindi cha Miaka mitano. Vipaumbele na uchaguzi wao,
uongozwe kwa namna ya pekee na Mafundisho Jamii ya Kanisa; utu na heshima ya binadamu,
mafao ya wengi; haki na amani. Wananchi wa Bara la Ulaya wanapaswa kushiriki kwa wingi
kabisa katika uchaguzi mkuu wa Jumuiya ya Ulaya kwani, tangu Mwaka 2008, Jumuiya ya
Kimataifa ilipojikuta inakabiliwa na mtikisiko wa uchumi kimataifa, watu wengi wamekata
tamaa na masuala ya kisiasa, kiasi kwamba, hawaoni tena sababu ya kushiriki kwenye
chaguzi mbali mbali.
Nchi wanachama wa Umoja wa Ulaya pamoja na wananchi katika
ujumla wao, wahakikishe kwamba, wanaweza kando masilahi ya nchi husika kwa kujikita
katika mafao ya wengi, ili kuwajengea watu matumaini yatakayowasaidia kukabiliana
na changamoto mbali mbali zinazoendelea kujitokeza kwa wakati huu, kwa kujikita katika
mshikamano wa upendo na udugu.
Baraza la Maaskofu wa COMECE linasema, kwamba,
sera na mikakati ya maendeleo kichumi na kijamii haina budi kwanza kabisa kuzingatia
utu na heshima ya binadamu, aliyeumbwa kwa sura na mfano wa Mungu. Maisha ni zawadi
kutoka kwa Mungu inayopaswa kuheshimiwa, kulindwa na kuendelezwa tangu pale mtoto
anapotungwa mimba tumboni mwa mama yake. Waamini na watu wote wenye mapenzi mema wasikubali
kumezwa na utamaduni wa kifo.
Ikumbukwe kwamba, familia ina umuhimu wake katika
maisha ya Kijamii na Kikanisa, kumbe, inapaswa kuheshimiwa na kusaidiwa kutekeleza
dhamana na majukumu yake barabara. Jumuiya ya Ulaya inapaswa kuboresha sera na mikakati
yake kuhusu wahamiaji na wageni wanaotafuta hifadhi ya maisha Barani Ulaya, kwa kuonesha
mshikamano wa dhati na nchi wanachama wa Jumuiya ya Ulaya.
Uhuru wa kidini
na umuhimu wa kuheshimu Jumapili kama siku ya mapumziko ni kati ya mambo ambayo yamegusiwa
pia na Maaskofu katika ujumbe wao, unaohitimishwa kwa kutoa mwaliko kwa wananchi wote
wa Umoja wa Ulaya kushiriki kikamilifu katika uchaguzi mkuu utakaofanyika kuanzia
tarehe 22 hadi 25 Mei, 2014.