2014-03-21 13:43:33

Rais George Abela wa Malta akutana na kuzungumza na Papa Francisko mjini Vatican


Baba Mtakatifu Francisko, Ijumaa tarehe 21 Machi amekutana na kuzungumza na Rais George Abela, Rais wa Malta ambaye baadaye alikutana na Kardinali Pietro Parolin, Katibu mkuu wa Vatican aliyekuwa ameambatana na Askofu mkuu Dominique Mamberti, Katibu mkuu wa mambo ya nchi za nje za ushirikiano wa kimataifa mjini Vatican.

Mazungumzo kati ya Baba Mtakatifu Francisko na mgeni wake yamefanyika katika hali ya utulivu kabisa kwa kupembua Ukristo katika historia, utamaduni na maisha ya wananchi wa Malta sanjari na uhusiano wa karibu kati ya Nchi hizi mbili, kama inavyojidhihirisha katika hija za kichungaji zilizofanywa na Mwenyeheri Yohane Paulo II na Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto XVI.

Kwa namna ya pekee mazungumzo ya viongozi hawa wawili yamejikita katika uhusiano kati ya Kanisa na Serikali ya Malta na mchango wa Kanisa katika sekta ya elimu na huduma za kijamii; mikataba iliyotiwa sahihi kati ya pande hizi kwa ajili ya ushirikiano na mafao ya wengi. Wamejadili mchango wa Malta katika Jumuiya ya Ulaya na Ukanda wa Mediterania, bila kusahau tatizo la wakimbizi linaloongezeka mwaka hadi mwaka. Wameangalia mchango wa Serikali na Kanisa katika kuwahudumia wahamiaji na watu wasiokuwa na makazi maalum.







All the contents on this site are copyrighted ©.