Rasilimali ya Nigeria ni kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya wengi!
Jumla ya wajumbe 492 kutoka katika medani mbali mbali za maisha nchini Nigeria, hivi
karibuni wamekutana na kufanya mazungumzo na Rais Goodluck Jonathan wa Nigeria kuhusu
umuhimu wa majadiliano ya kitaifa kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya Nigeria katika
ujumla wake. Mchakato huu hauna budi kwenda sanjari na ugavi na matumizi bora ya rasilimali
ya Nigeria kwa ajili ya mafao ya wengi.
Mkutano wa kitaifa unalenga pamoja
na mambo mengine kujenga na kukuza matumaini mapya, umoja na mshikamano wa kitaifa.
Wajumbe wanapenda kuona kwamba, rasilimali na utajiri wa taifa unatumika kwa ajili
ya mafao ya wengi pamoja na kudhibiti madaraka ya Rais wa Nigeria. Wajumbe hawa ni
kielelezo cha uwakilishi mpana zaidi wa kitaifa kwa ajili ya mafao ya taifa zima.
Mkutano huu unafanyika wakati huu ambapo bado kuna mashambulizi ya watu wasiokuwa
na hatia pamoja na uharibifu mkubwa wa mali na miundo mbinu.
Majadiliano ya
kitaifa kwa ajili ya mafao na maendeleo ya Nigeria ni wazo ambalo liliwahi kufanyiwa
kazi kunako Mwaka 2004, wakati wa utawala wa Rais Olusegun Obasanjo. Wazo la Rais
Goodluch Jonathan la kutaka kugombea Urais kwa awamu ya tatu limeanza kuzua kichefuchefu
miongoni mwa wananchi wa Nigeria.