2014-03-18 09:23:14

Mapambano dhidi ya baa la njaa!


Shirika la Misaada la Kanisa Katoliki Ureno, kuanzia tarehe 17 hadi tarehe 23 Machi 2014 linaadhimisha Juma la Kupambana na Baa la Njaa Kitaifa linaloongozwa na kauli mbiu "Mshikamano wa upendo dhidi ya baa la njaa". Caritas Ureno inatumia kipindi hiki kwa ajili ya kuhamasisha mshikamano wa upendo na udugu katika mchakato wa kupambana na baa la njaa duniani.

Kati ya tarehe 20 hadi tarehe 23 Machi 2014, Caritas itakusanya mchango kutoka kwa waamini na watu wenye mapenzi mema kwa ajili ya kugharimia miradi mbali mbali inayoendeshwa na Kanisa Katoliki nchini Ureno. Waamini na wananchi wote kwa ujumla, wanachangamotishwa kuhakikisha kwamba, wanashiriki kikamilifu katika ujenzi wa jamii inayosimikwa katika haki, upendo na mshikamano wa kidugu. Kila mwananchi akitekeleza dhamana na wajibu wake ndani ya Jamii, kuna uwezekano mkubwa wa kupata mafao ya wengi.

Caritas Ureno inaungana na Shirikisho la Mashirika ya Misaada ya Kanisa Katoliki Kimataifa, Caritas Internationalis katika kampeni dhidi ya baa la njaa duniani ifikapo mwaka 2025. Hii ni Kampeni inayoongozwa na kauli mbiu "Familia moja ya binadamu, chakula kwa wote" iliyozinduliwa Desemba 2013 kwa kumshirikisha Baba Mtakatifu Francisko aliyetuma ujumbe wake kwa njia ya Video.







All the contents on this site are copyrighted ©.