2014-03-18 12:19:52

Jumuiya ya Kimataifa ikijizatiti, baa la njaa litapewa kisogo!


Bwana Kanayo Nwanze, Rais wa Mfuko wa Maendeleo ya Kilimo wa Umoja wa Mataifa, IFAD katika mahojiano maalum na Radio Vatican anabainisha kwamba, Baba Mtakatifu Francisko ni kiongozi ambaye anaguswa na baa la njaa duniani, jambo ambalo linajionesha katika historia na maisha yake adili na manyofu. Ni kiongozi anayeendelea kuichangamotisha Jumuiya ya Kimataifa kuleta mabadiliko katika maisha ya watu, kwa kuguswa na mateso ya watu wanaoteseka kwa baa la njaa duniani.

Bwana Nwanze anasema, asilimia 30% ya chakula kinatupwa sawa na kutupa mabillioni ya fedha ambayo ingeweza kutumika kuganga baa la njaa duniani. Takwimu zinaonesha kwamba, asilimia 20 hadi 40% ya chakula kinachozalishwa inapotea njiani kabla hata ya kumfikia mlaji. Hapa kunaonesha jinsi ambavyo chakula kinavyopotea na kutupwa na wakati huo huo, Jumuiya ya Kimataifa inasema kwamba, kuna haja ya kujifunga kibwebwe ili kuongeza uzalishaji wa chakula kwa watu billioni 9 ifikapo mwaka 2050.

Chakula kinachozalishwa duniani kwa wakati huu kina uwezo wa kutosheleza mahitaji ya watu billioni 7.1. Jambo linalokwamisha upatikanaji wa chakula kwa watu wengi zaidi ni ubovu wa miundo mbinu ya barabara hasa vijijini na katika nchi zile ambazo zimeathirika vibaya kutokana na mabadiliko ya tabianchi.

Baba Mtakatifu Francisko anaendelea kutoa changamoto kubwa kwa Jumuiya ya Kimataifa kushikamana kama binadamu na kwamba, ni jambo lisilokubalika kwamba, watu zaidi ya billioni 1 waendelee kuteseka kutokana na utapiamlo na baa la njaa. Mashirika ya Misaada ya Umoja wa Kimataifa yanadhamana na wajibu wa kuwapatia wananchi furaha sanjari na kuwajengea uwezo ili waweze kupambana na baa la njaa, umaskini na maradhi.

Wakulima wadogo wadogo wajengewe uwezo katika uzalishaji wa mazao ya chakula na biashara; ili kuwa na uhakika wa usalama wa chakula na pato kwa ajili ya kuboresha hali ya maisha ya familia husika.







All the contents on this site are copyrighted ©.