Changamoto zinazoendelea kufanyiwa kazi na Papa Francisko!
Tangu Baba Mtakatifu Francisko alipochaguliwa kuliongoza Kanisa mwaka mmoja uliopita
amejielekeza zaidi katika kutoa kipaumbele cha kwanza kwa maskini na wote wanaosukimizwa
pembezoni mwa Jamii; haki, amani, upendo na mshikamano wa kidugu kati ya watu wa mataifa,
kwa kuguswa na mahangaiko ya watu wanaowazunguka.
Papa ameendelea kuombea
amani na upatanisho kati ya mataifa na kwamba, majadiliano ya kina yawe ni msingi
wa kutafuta ufumbuzi wa matatizo na changamoto zinazoendelea kuukabili ulimwengu.
Mahangaiko ya watu wasiokuwa na hatia huko Sudan ya Kusini bila kusahau sehemu ambazo
kwa sasa zinakabiliana na vita pamoja na kinzani za kijamii ni kati ya mambo ambayo
yanamgusa Baba Mtakatifu kwa sasa.
Hayo yamesemwa hivi karibuni na Askofu mkuu
Charles Daniel Balvo, Balozi wa Vatican nchini Kenya, katika hafla ya kumbu kumbu
ya Mwaka mmoja, tangu Baba Mtakatifu Francisko alipochaguliwa kuliongoza Kanisa Katoliki.
Upendo na mshikamano; haki, amani, upatanisho na msamaha wa kweli, ni changamoto inayoendelea
kutolewa na Baba Mtakatifu Francisko kwa ajili ya maisha na utume wa Kanisa na Jamii
katika ujumla wake.
Kanisa linapaswa kuendelea kujikita katika ukweli, haki,
amani na uhuru kamili katika utekelezaji wa dhamana na utume wake sehemu mbali mbali
za dunia, kwa ajili ya mafao ya wengi na ustawi wa Jamii husika. Baba Mtakatifu Francisko
alichaguliwa hapo tarehe 13 Machi 2013 na kuanza rasmi utume wake kama Khalifa wa
Mtakatifu Petro hapo tarehe 19 Machi 2013 sanjari na Siku kuu ya Mtakatifu Yosefu,
Mchumba wa Bikira Maria na Mlinzi wa Kanisa.
Wakati huo huo, Serikali ya Kenya
imelipongeza Kanisa kwa kushiriki kikamilifu katika mchakato wa kuwaletea wananchi
wa Kenya maendeleo endelevu yanayomgusa mtu mzima: kiroho na kimwili. Kanisa limeendelea
kuwa mstari wa mbele katika sekta ya elimu, afya na maendeleo endelevu, hasa katika
maeneo ya vijijini. Kanisa Katoliki nchini Kenya linamiliki na kuendesha shule za
msingi na sekondari 8, 000. Kanisa lina vyuo vikuu na taasisi za elimu ya juu 5. Kanisa
lina hospitali, vituo vya afya na zahanati zaidi ya 500 pamoja na vituo 5 kwa ajili
ya watoto yatima.
Maendeleo ya sekta ya elimu nchini Kenya ni mchango mkubwa
uliotolewa na unaoendelea kutolewa na Kanisa, sanjari na kuhakikisha kwamba, huduma
hii inazingatia ubora na viwango vya kitaifa na kimataifa. Serikali ya Kenya inasema
kwamba, itaendelea kushirikiana na Kanisa katika kulinda na kutetea: haki na amani;
maendeleo na ustawi wa wananchi wote wa Kenya