2014-03-15 08:27:15

Mkristo unaalikwa kwenda Jangwani!


Padre Raniero Cantalamessa, mhubiri wa nyumba ya Kipapa, katika mahubiri ya Kipindi cha Kwaresima yaliyofanyika kwenye Kikanisa cha Redemptoris Mater mjini Vatican Ijumaa tarehe 14 Machi 2014 amekazia mambo makuu yafuatayo: umuhimu wa jangwa katika maisha ya kiroho; aina mpya za kufunga na kusali zinazokubalika mbele ya Mwenyezi Mungu; majaribu katika maisha na umuhimu wa waamini kumfuasa Yesu katika Jangwa la maisha yao, ili kufunga, kusali na kutafakari kwa kina Neno la Mungu.

Padre Cantalamessa anasema, mwaliko wa kumfuasa Yesu Jangwani ni kwa ajili ya Wakristo wote ingawa kuna baadhi ya Wamonaki walioguswa kwa namna ya pekee wakaacha yote na kujitenga na malimwengu kwa ajili ya kusali na kulitafakari Neno la Mungu. Kila mwamini anapaswa kuchagua Jangwa la maisha yake ya kiroho, ili kuweza kuingia katika undani wa maisha yake, ili hatimaye, aweze kugundua ile sura na mfano wa Mungu iliyo ndani mwake, kwa kukazia mambo msingi katika maisha.

Hii ni changamoto ya kujenga na kukuza amani na utulivu wa ndani ili kutoa kipaumbele cha kwanza kwa Mwenyezi Mungu. Kwenda Jangwani kuna maanisha kutenga muda maalum kwa ajili ya kusali na kulitafakari Neno la Mungu, tayari kuanza hija mpya ya maisha ya kiroho.

Padre Cantalamessa anasema kufunga kunakokubalika mbele ya Mwenyezi Mungu kunajikita katika kwanza kabisa kuguswa na mahangaiko ya wengine, tayari kuwashirikisha kile ambacho Mwenyezi Mungu amekukirimia katika maisha kwa njia ya matendo ya huruma na mapendo. Ni hali ya kujinyima kwa ajili ya wengine pamoja na kudhibiti vilema vya maisha ya binadamu, ili kuomba huruma na upendo wa Mungu usiokuwa na mipaka.

Kufunga ni sehemu ya mchakato wa utekelezaji wa haki jamii kwa kuwasaidia wengine kuweza kupata maisha bora zaidi ili kuondokana na baa la njaa, ujinga na maradhi. Ni harakati za kujenga na kudumisha misingi ya haki, amani, upendo na mshikamano kama kielelezo cha imani tendaji inayomwilishwa katika uhalisia wa maisha ya mwamini.

Padre Cantalamessa anasema, Yesu alipokuwa Jangwani akifunga na kusali kwa siku arobaini alijaribiwa na Shetani. Uwepo wa Pepo wachafu ni jambo ambalo linawakumba watu wengi wa nyakati hizi, kiasi cha kuwafanya kuwa ni mateka wa imani za kishirikina ambazo kimsingi zimekuwa ni chanzo hata cha maafa ya watu wasiokuwa na hatia sehemu mbali mbali za dunia. Wakristo wanafundishwa kwamba, Yesu alimshinda mwovu Shetani kwa njia ya Msalaba, ili kutekeleza kazi ya ukombozi aliyokuwa amedhaminishwa na Baba yake wa mbinguni.

Yesu alitekeleza kazi ya ukombozi kwa njia ya utii, unyenyekevu na mateso makali, kinyume kabisa na Shetani aliyekuwa anamtaka Yesu kuchukua njia ya mkato katika utekelezaji wa kazi ya ukombozi. Shetani anajitokeza katika mambo ambayo yanamvuto na mashiko kwa binadamu kama vile: fedha na utajiri wa haraka haraka; madaraka na sifa kemkem; chakula, vinywaji pamoja na ngono! Waamini wakiendekeza mambo haya wataweza kujikuta wametumbukizwa pabaya katika maisha yao!

Padre Cantalamessa anasema, baada ya Yesu kubatizwa Mto Yordan alikwenda Jangwani ili kusali na kufunga kwa kutoa kipaumbele cha kwanza kwa uwepo wa Mungu katika maisha na utume wake. Hili ndilo fundisho kubwa linalotolewa kwa Wakristo wakati huu wa Kwaresima, kwamba, kuna haja kila mara kuhakikisha kwamba, wanajitenga na malimwengu kwa ajili ya kusali, kufunga na kutfakari Neno la Mungu, kama njia ya kujichotea nguvu ya maisha ya kiroho, tayari kupambana na changamoto mbali mbali zinazojitokeza katika maisha.

Jangwa ni mwaliko wa kuingia katika undani, ili kuzungumza na Mwenyezi Mungu, katika ukweli na haki. Hata leo hii anasema Padre Raniero Cantalamessa, Yesu bado anawasubiri wafuasi wake katika Jangwa la maisha ya miyo yao, kamwe wasimwache pweke!







All the contents on this site are copyrighted ©.