Kumbu kumbu ya miaka 450 ya Wamonaki kwenye Monasteri ya Quattro Coronati, Roma
Baba Mtakatifu Francisko katika ujumbe ulioandikwa kwa niaba yake na Kardinali Pietro
Parolin, Katibu mkuu wa Vatican katika Maadhimisho ya Kumbu kumbu ya Miaka 450 ya
uwepo wa Wamonaki wa Mtakatifu Agostino kwenye Monasteri ya Mtakatifu Quattro Santi
Coronati, iliyoko Jimbo kuu la Roma, anaendelea kuwatia shime katika maisha na utume
wa Kanisa sehemu mbali mbali za dunia, hasa zaidi mahali ambako Kanisa linakabiliana
na madhulumu, ili waamini waweze kupata faraja kutoka kwa Mwenyezi Mungu.
Kardinali
Agostino Vallini, Makamu Askofu Jimbo kuu la Roma ameadhimisha Ibada ya Misa Takatifu
kama kielelezo cha shukrani kwa Mwenyezi Mungu kwa kuwawezesha Wamonaki, kunako tarehe
12 Machi 1564 kuanza maisha yao kwenye Monasteri hii, ambayo wakati wa Vita kuu ya
Pili ya Dunia, ilitoa hifadhi kwa maelfu ya Wayahudi, kama ilivyokuwa imeelekezwa
na Papa Pio wa kumi na mbili. Baba Mtakatifu Francisko anawaalika Wamonaki hawa kumsindikiza
katika maisha na utume wake kwa njia ya sala na majitoleo yao ya kila siku.