2014-03-15 07:38:20

Cor Unum, kielelezo cha mshikamano wa upendo kwa waathirika wa maafa duniani


Baraza la Kipapa linaloratibu misaada ya Kanisa Katoliki, Cor Unum ndicho kitengo maalum cha misaada inayotolewa na Kanisa Katoliki kwa watu kutoka sehemu mbali mbali duniani. Kwa maneno mengine, Cor Unum ndio mkono wa upendo wa Baba Mtakatifu kwa watu wanaokabiliana na maafa sehemu mbali mbali za dunia. RealAudioMP3

Baraza hili lilianzishwa na Papa Paulo VI kunako tarehe 15 Julai 1971 na tangu wakati huo, Cor Unum limekuwa mstari wa mbele katika kuwahudumia watu kiroho na kimwili kama kielelezo cha mshikamano wa huruma na upendo unaobubujika kutoka kwa Kristo na Kanisa lake.

Hivi ndivyo anavyobainisha Askofu mkuu Giampietro Dal Tosso, Katibu mkuu wa Baraza la Kipapa linaloratibu misaada ya Kanisa Katoliki, Cor Unum katika mahojiano maalum na Gazeti la L’Osservatore Romano, linalomilikiwa na Vatican. Cor Unum ni kielelezo makini cha udugu na mshikamano wa mapendo unaooneshwa na Mama Kanisa kwa watu wanaoteseka: kiroho na kimwili; watu wanaokabiliana na maafa asilia, vita na majanga mengine ya maisha.

Kwa Mwaka 2013, Kanisa limeonesha mshikamano wa huruma na mapendo kwa wananchi wa Ufilippini waliokumbwa na tufani kubwa iliyopelekea maelfu ya watu kupoteza maisha na mali zao. Kanisa bado linaendelea kuchangia kwa hali na mali nchini Syria ambako kuna maelfu ya watu wasiokuwa na hatia wanaendelea kupoteza maisha yao na wengine wanalazimika kuyakimbia makazi yao kwa kuhofia usalama wa maisha na mali zao. Idadi inaonesha kwamba, kuna wakimbizi zaidi ya millioni sita kutoka Syria wanaohitaji msaada wa hali na mali.

Licha ya Baba Mtakatifu Francisko kuwasindikiza wananchi wa Syria kwa njia ya sala na kufunga, kama alivyofanya hapo tarehe 7 Septemba, 2013, bado Mashirika mbali mbali ya Misaada ya Kanisa Katoliki yanashiriki kusaidia kutoa huduma kwa wananchi wa Syria na kwa nchi jirani.

Kuna zaidi ya Mashirika 25 yaliyoko chini ya mwamvuli wa Kanisa Katoliki yanayotoa misaada ya kiutu huko Mashariki ya Kati. Mashirika haya yanasaidiana kutoa huduma makini kwa wananchi wa Syria bila ya ubaguzi wala upendeleo wa kisiasa, kidini au mahali anapotoka mtu! Wote wanapata huduma sawa sawa kwani wameumbwa kwa sura na mfano wa Mungu.

Mashirika ya Misaada ya Kanisa Katoliki yanaendelea pia kutoa huduma ya kiutu kwa wakimbizi na wahamiaji wanaoishi nchini Lebanon. Cor Unum ina mpango mkakati wa kuanzisha hospitali kwa ajili ya watoto wadogo nchini Lebanon, itakayokuwa inashirikiana na Hospitali ya Bambino Gesù inayomilikiwa na Vatican, ili kutoa huduma kwa watoto huko Mashariki ya Kati, hasa kwa ajili ya kuwahudumia watoto wa wakimbizi kutoka Syria.

Askofu mkuu Giampietro dal Tosso anasema, huduma ya upendo ni asili ya Kanisa kama ambavyo anabainisha Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto wa kumi na sita; kwani inawahusisha waamini katika uhuru wao kama wafuasi wa Kristo wenye dhamana ya kushuhudia imani katika matendo kwa kushirikiana na viongozi wa Kanisa, ili yote yafanyike kwa ajili ya sifa na utukufu wa Mungu.

Maaskofu mahalia hawana budi kuhakikisha kwamba, wanaratibu huduma na misaada inayotolewa na Mama Kanisa kwa kuzingatia misingi ya ukweli na uwazi; upendo na mshikamano wa dhati kati ya watu! Hii ni huduma inayotolewa kwa kuzingatia Mafundisho Jamii ya Kanisa, lengo ni kushuhudia imani kwa njia ya huduma ya upendo. Cor Unum imepewa dhamana na Mama Kanisa kuhakikisha kwamba, inaratibu misaada ya Kanisa Katoliki kwa kushirikiana na Mashirika mbali mbali ya Misaada ya Kanisa Katoliki yaliyoenea sehemu mbali mbali za dunia.

Askofu mkuu Giampietro Dal Tosso anasema, Mfuko wa Yohane Paulo II kwa ajili ya Sahel pamoja na Mfuko wa Maendeleo ya watu Amerika ya Kusini, ni mashirika mawili ambayo yanasimamiwa moja kwa moja na Cor Unum, katika mchakato wa kudhibiti kuenea kwa Jangwa la Sahara, Barani Afrika sanjari na kusaidia mbinu mkakati wa maendeleo na majiundo kwa wananchi wa Amerika ya Kusini.

Mwaka 2014 kutafanyika mkutano wa viongozi wakuu wa Mfuko wa Maendeleo ya watu Amerika ya Kusini, ili kuangalia vipaumbele kadiri ya maagizo ya Kanisa kwa ajili ya wananchi wa Amerika ya Kusini.

Imehaririwa na
Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.








All the contents on this site are copyrighted ©.