Baba Mtakatifu Francisko ameadhimisha kumbu kumbu ya Mwaka mmoja tangu alipochaguliwa
kuliongoza Kanisa Katoliki kwa sala na mafungo ya kiroho. Hata hivyo amepokea salam
na matashi mema kutoka sehemu mbali mbali za dunia kutokana na mchango wake katika
maisha na utume wa Kanisa katika mapambazuko ya Millenia ya tatu ya Ukristo.
Kati
ya viongozi wa kimataifa waliotuma salam zao ni pamoja na Rais Giorgio Napolitano
wa Italia anayekiri kwamba, maisha na utume wa Baba Mtakatifu Francisko umewagusa
watu wengi ndani na nje ya Kanisa Katoliki. Papa anaonesha upendeleo wa pekee kwa
maskini na wote wanaoteseka kutokana na ukosefu wa misingi ya haki, amani na usawa.
Mwanadamu na haki zake msingi anapaswa kupewa kipaumbele cha kwanza.
Patriaki
wa Kanisa la Kiorthodox Mosco, Cyril anampongeza Baba Mtakatifu Francisko kwa kutoa
kipaumbele cha pekee katika majadiliano ya kiekumene, ili kujenga na kudumisha umoja
na mshikamano miongoni mwa Wakristo; mambo ambayo yamejionesha kwa namna ya pekee,
tangu alipochaguliwa kuliongoza Kanisa Katoliki.
Professa Foad Aodi kwa niaba
ya Jumuiya ya Waamini wa dini ya Kiislam wanaoishi nchini Italia ametuma pia salama
na matashi mema kwa Baba Mtakatifu Francisko, kwa kuwa makini katika majadiliano ya
kidini yanayopania kujenga na kudumisha: haki, amani, upendo na upatanisho wa kweli.
Baraza la Maaskofu Katoliki Canada linampongeza Baba Mtakatifu kwa msukumo
wake wa pekee kwa Kanisa kuwaendelea watu wanaoishi pembezoni mwa Jamii, ili kuwaonjesha:
Injili ya Furaha, Huruma na Upendo wa Mungu kwa watu. Jitihada za kudumisha dhamana
na utume wa Familia ndani ya Kanisa na Jamii katika ujumla wake, ambazo zimevaliwa
njuga na Baba Mtakatifu Francisko wakati huu ni kati ya mambo ambayo wanaendelea kumshukuru
ili Kanisa liweze kutoa majibu muafaka kwa changamoto mbali mbali zinazoendelea kujitokeza
katika mikakati yake ya kichungaji.
Baraza la Maaskofu Katoliki Ireland linasema:
huruma na upendo wa Mungu ni kati ya kauli mbiu zinazofanyiwa kazi na Baba Mtakatifu
Francisko katika maisha na utume wake, mwaliko wa kuendelea kutangaza Injili ya Furaha,
ili kuwawezesha kukutana na Yesu Kristo anayewakomboa kutoka katika dhambi na mauti;
anayewapatia furaha ya ndani na faraja kutokana na upweke hasi wanaokumbana nao katika
maisha yao ya kila siku. Changamoto kwa Wakristo kujifunga kibwebwe katika mchakato
wa Uinjilishaji Mpya ni dhana inayofanyiwa kazi na Kanisa Katoliki nchini Ireland.
Maaskofu Katoliki Ireland wanamtakia kheri na baraka Baba Mtakatifu Francisko katika
maisha na utume wake.
Baraza la Maaskofu Katoliki Italia linasema, linaendelea
kumsindikiza Baba Mtakatifu Francisko kwa njia ya sala katika maisha na utume wake
kama Khalifa wa Mtakatifu Petro. Wanaunga mkono changamoto ya toba na wongofu wa ndani
pamoja na kuendelea kukuza ari na moyo wa Kimissionari ndani ya Kanisa, ili kujenga
na kudumisha umoja, upendo na mshikamano wa kidugu ndani ya Kanisa. Kanisa Katoliki
nchini Italia linapenda kushikamana na Baba Mtakatifu Francisko katika utume wake
kwa Kanisa la Kiulimwengu.