Waziri mkuu wa Tanzania Mizengo Pinda aagiza huduma za upimaji wa figo zitolewe kwa
kuzunguka katika kanda zilipo nchini na kuacha utamaduni wa kutoa huduma hizo wakati
wa maadhimisho hayo tuu. Alisema hayo Alhamisi, tarehe 13 Machi 2014 wakati wa akifunga
kilele cha Maadhimisho ya Wiki ya Afya ya Figo Duniania yaliyofanyika katika Viwanja
vya Nyerere mkoani Dodoma, yenye kauli mbiu Figo Huzeeka kama wewe. Jali Afya ya Figo
zako.
Akizungumza na wananchi wakati wa kilele hicho Waziri Mkuu aliwaeleza
wananchi kujenga utamaduni wa kujali na kupima afya zao mara kwa mara: ‘‘Tumieni fursa
hii ya uwepo wa huduma hizi karibu nanyi kujua hali ya afya ya figo zenu ili mchukue
hatua stahiki mapema, kuchelewa kujua afya yako kunaweza kuathiri pia urahisi wa matibabu
kama ukigundulika kwamba umeathirika na Ugonjwa wa Figo“.
Alisema, huduma
kama hizi za Klinic ya Umma yaani Public Clinic zitolewe mara kwa mara kikanda bila
kusubiria maadhimisho ili kuweza kuwafikia wananchi kwa wakati na kuendelea kuhamasisha
huduma za afya za aina hii kwa wananchi, walau kuweza kutoa huduma hizi katika Kanda
ya juu Kusini, Kanda ya Ziwa, Kanda ya Magharibi na Kanda ya Kaskazini mtakuwa mmefanya
jambo la busara sana kwa watanzania.
Waziri Pinda alisema, zipo njia muhimu
za kuzingatia ili kuepukana na ugonjwa wa figo kama inavyoelezwa na wataalum kuwa
ni pamoja na kufanya mazoezi kwa wingi, kunywa maji glass 6 hadi 8 kila siku, kuacha
kuvuta sigara, kuzingatia uzito wa mwili na kuacha kutumia dawa kabla ya maelekezo
ya daktari, aliongezea Waziri Pinda.
Waziri Mkuu alisema, ‘‘Dawa hapa ni Kinga
na Sio Tiba“ hivyo aliwaomba wananchi kujenga utamaduni wa kupima afya zao mara kwa
mara ili kuweza kufahamu na kupunguza madhara makubwa ya ugonjwa huu.
Changamoto
kubwa iliyopo mbele yetu kama serikali ni upungufu wa madaktari bingwa wa kutosha
wa kutibu magonjwa ya figo, kupandikiza figo na gharama kubwa za matibabu ya figo
ambayo huduma hiyo haipatikani hapa nchi hivyo: ‘‘Serikali itachukua jukumu la kuongeza
idadi ya wataalamu wa figo na kwa kuzingatia suala hili tutaliweka katika bajeti ya
Serikali ya mwaka“, alisema Waziri Mkuu.
Alieendelea kusema kuwa, kuna Sera
ya Magonjwa ya Afya ya mwaka 2007, Miongozo na Mikakati ya kupambana na ugonjwa huu
hivyo, Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii kwa kushirikiana na Taasisi ya Taifa ya Figo
Tanzania, itazindua ripoti ya Wiki ya Afya ya Figo 2013 Tanzania, ambapo ripoti hiyo
itaonesha kuwa watu 4,325 walijitokeza kupima afya za figo zao na kati ya hao asilimia
15 (623/325) walipatikana na matatizo ya figo.
Ni dhahiri kuwa, juhudi hizi
za kubaini ukubwa wa tatizo la ugonjwa wa Figo, zinazofanywa na Serikali zitarahisisha
na kuwezesha wananchi wengi kupata taarifa mbalimbali kutoka ndani na nje ya Nchi
kuhusu afya ya figo.
Pamoja na kuhudhuria Kilele cha maadhimisho hayo, Waziri
Mkuu alizindua rasmi tovuti ya Taasisi ya Taifa ya Figo ambayo itakuwa inalezea masuala
yote yanayohusu figo na kusisitiza wananchi kutumia tovuti hiyo kujifunza masuala
yote masuala mbalimbali ya figo.
Mapema, Prof. Ephata Kaaya, ambaye ni Mjumbe
wa Bodi Taasisi ya Taifa ya Figo alieleza kuwa dira na malengo ya taasisi hiyo ni
kuwa kitovu cha taifa katika kuendeleza na kuthibiti magonjwa ya figo kwa kuendelea
kutoa elimu kwa wingi, kufanya tafiti mbalimbali ili kuweza kufaham takwimu halisi
za ugonjwa huo, kwani katika maadhimisho haya jumla ya wananchi 3800 wameweza kusajiliwa
na wananchi 3120 wamefanyiwa uchunguzi.
Taasisi ya Taifa ya Figo itaendelea
kushirikiana na Wizara ya Afya, Sekta Binafsi na wananchi kuendesha masuala ya matibabu
ya figo na kubuni mbinu mbadala ya upatikanaji wa fedha ili kuweza kuendesha Taasisi
hiyo ambayo hivi sasa inatoa huduma za matibabu ya figo katika Hospitali ya Taifa
Muhimbili, Hospitali ya Rufaa Mbeya, na huduma hizo pia zitaanzishwa katika Hospitali
za Rufaa Bugando na KCMC.