2014-03-14 12:00:35

Askofu Dallu ateuliwa kuwa Askofu mkuu wa Jimbo kuu la Songea, Tanzania


Baba Mtakatifu Francisko amemteua Askofu Damian Denis Dallu wa Jimbo Katoliki Geita, Tanzania kuwa Askofu mkuu wa Jimbo kuu la Songea. Itakumbukwa kwamba, Askofu mkuu mteule Dallu alizaliwa kunako Mwaka 1956 huko Kiponzelo, Jimbo Katoliki la Iringa. RealAudioMP3

Baada ya masomo na majiundo yake ya Kikasisi, akapadrishwa tarehe 15 Novemba 1984. Tarehe 6 Mei 2000 akateuliwa kuwa ni Askofu wa Jimbo Katoliki la Geita, Tanzania. Askofu Dallu aliwekwa wakfu na hatimaye kusimikwa kuwa ni Askofu wa pili wa Jimbo la Geita hapo tarehe 30 Julai 2000.

Katika mahojiano maalum na Radio Vatican, Askofu mkuu mteule Dallu anazungumzia umuhimu wa Katekisimu Mpya ya Kanisa Katoliki kama muhtasari wa imani inayoungamwa na kuadhimishwa na Mama Kanisa. Hii ni imani inayomwilishwa katika maisha adili kwa kufuata Amri za Mungu na kumwilishwa katika sala. Katekisimu Mpya ya Kanisa Katoliki imetoa kipaumbele cha pekee katika Mafundisho Jamii ya Kanisa kwa kutoa kipaumbel cha kwanza kwa binadamu na haki zake msingi.

Askofu mkuu mteule Damin Denis Dallu anasema, Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican ni nyenzo msingi katika maisha na utume wa Kanisa katika kukabiliana na changamoto mbali mbali za kichungaji katika ulimwengu mamboleo. Ni mwaliko kwa Kanisa kukuza na kudumisha majadiliano ya kidini na kiekumene ili kujenga misingi ya haki na amani kwa Familia nzima ya binadamu. Kumbe, Katekisimu Mpya ya Kanisa Katoliki na Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican ni mafundisho mfungamano kwa binadamu wote.







All the contents on this site are copyrighted ©.