2014-03-13 12:00:47

Wajibu wa kuuishi, kuulinda na kuusimamia ukweli kishuhuda!


Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican inakuletea sehemu ya pili ya Ujumbe wa Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania katika kipindi cha Kwaresima kwa Mwaka 2014. Mara ya mwisho, tuliwashirikisha utangulizi, leo tunaendelea na sura ya kwanza inayopembua wongofu wa kweli unaomweka mtu huru na sehemu ya pili inajadili wajibu wa kuuishi, kuulinda na kusimamia ukweli kishuhuda. Ndani ya viunga vya Radio Vatican kukujuza zaidi ni Sr. Gisela Upendo Msuya. RealAudioMP3
SURA YA KWANZA
WONGOFU WA KWELI HUTUWEKA HURU

Mungu alipenda kujifunua kwa wanadamu kupitia manabii na mwanawe wa pekee Bwana wetu Yesu Kristo. Hata leo, Roho Mtakatifu analiongoza Kanisa katika kuendelea kuujua ukweli wa kiimani katika safari ya pamoja ya kiroho kuelekea uhuru kamili wa roho zetu. Ukweli wa kiimani huleta uhuru wa kiroho. Mwaka uliopita Kanisa liliadhimisha Mwaka wa Imani ikiwa ni sehemu ya kuwakumbusha wanakanisa wote juu ya wajibu wao wa kiimani katika Kanisa na katika jamii.

Kwa kuishi ipasavyo imani yetu ya kikristo tunashiriki wajibu wa kuujenga Ufalme wa Mungu ambao mojawapo ya nguzo zake saba za msingi ni ukweli! Hakika, ufalme wa Mungu, kama Mama Kanisa anavyotangaza katika utangulizi wa Misa ya sherehe ya Kristo Mfalme ni ufalme wa UZIMA na KWELI, ufalme wa NEEMA na UTAKATIFU, ufalme wa HAKI, MAPENDO na AMANI. Mungu wetu ni UKWELI na ni MKWELI. Tunasadiki na kukiri kwamba hadaganyi wala hadanganyiki. Imani ni wajibu wa kushiriki kuujenga Ufalme wa Mungu, ufalme ambao msingi wake ni ukweli, kwa sababu Mungu ni ukweli.

Mwanadamu aliyekombolewa kwa damu ya thamani kubwa sana ya Kristo iliyomwagika pale Kalvari, amepata kurudishiwa hadhi ya kuwa mwana huru wa Mungu akikombolewa kutoka utumwa wa dhambi. Uhuru anaoupata mwanadamu una gharama kubwa na thamani kubwa. Uhuru wa kweli ni uhuru ndani ya Mungu; ni uhuru katika Mungu. Uhuru wa kweli huambatana na utii wa sheria ya Mungu na uwajibikaji unaodai unyenyekevu na nidhamu ya hali ya juu. Uhuru huu ni kinyume na uhuru usio na mipaka ambao jamii ya sasa inadai,uhuru ambao hupingana na malengo ya Muumba na taratibu na miongozo halali mbele za Mungu iliyowekwa na jamii.

Kanisa, ukweli na uhuru

Kanisa ambalo ni ishara ya wokovu na alama ya uwepo hai wa Kristo aliye njia, ukweli na uzima katika ulimwengu wa sasa ni sisi tulioalikwa kuwa Familia ya Mungu. Kwa kumkiri Kristo na kwa kubatizwa kwetu tumekuwa Rafiki na wadau wake Yesu Kristo (Yn 15: 14). Kwa namna hiyo sisi sote Familia ya Mungu – Wakleri, Watawa na Waumini Walei – tu chombo mikononi mwa Kristo kwa kushiriki kikamilifu kazi ya Kristo ya kuwakomboa watu.

Kwa mantiki hiyo, Kanisa linao wajibu wa kwanza kabisa kuulinda ukweli, kuusimamia, kuushi na kuutangaza. Kanisa ni chombo kiletacho wokovu kwa ulimwengu na kuwaweka huru wanadamu walio katika utumwa unaojidhihirisha katika sura mbalimbali kama vile, umasikini, ufisadi, rushwa, ushirikina, magonjwa, siasa chafu, kutokuwajibika, ubinafsi,nk.

Kanisa ni chombo cha Kristo cha kuwaletea watu uhuru wa kweli. Roho wa Bwana, aliye juu ya Yesu (Lk 4:18,19) yuko pia juu ya Kanisa lake ambalo analituma kuwafungulia watu vifungo vyao mbalimbali na kuwaachia huru waliosetwa (Lk 4:18-19).

Ukweli kama tunu ya kimungu lazima uote mizizi katika mioyo ya wanadamu walioumbwa kwa sura na mfano wake (Kut 1:26). Ni wajibu wa kila mwanadamu kuutafuta ukweli na kuujua. Kwa njia ya ufahamu, mwanadamu anaalikwa kuutafuta ukweli kwani ndio njia pekee ya kumweka huru na kuufikia wokovu. Maana Mungu amemwachia mwanadamu uhuru kusudi aifuate nia yake (YBS 14:15), na hivyo amtafute Muumba wake kwa hiari, na hatimaye aufikie ukamilifu ulio bora na wenye heri, pasipo shuruti na kwa kuambatana na Mungu. Kanisa linamsaidia mwandamu kufanikisha kuufikia ukweli na kwa uhuru kupitia neema za Mungu.

SURA YA PILI
WAJIBU WA KUUISHI, KUULINDA NA KUUSIMAMIA UKWELI KISHUHUDA

Waamini waliowekwa huru na Kristo, wanao wajibu wa kuujua ukweli, kuutafuta, kuulinda na kuusimamia kwa lengo la kuleta huru wa kweli kwa manufaa ya wote. Huko ndiko kuwa mfuasi wa Kristo aliyesema: “Mimi nilikuja ulimwenguni; ili niishuhudie kweli. Kila aliye wa hiyo kweli hunisikia sauti yangu” (Yn 18:38).

Jamii leo hii imegawanyika juu ya uhuru ambao wanajamii wanapaswa kuwa nao. Wazazi wanaamini kuwa uhuru ni kutenda jambo lolote bila kubughudhiwa na yeyote, hata kama tendo hilo ni kinyume na misingi ya maadili. Watoto wanataka uhuru binafsi katika kupanga na kuamua mambo yanayowahusu. Watoto wasingependa kupokea malezi na maelekezo iwe ni ya wazazi au ya jamii. Vijana wanapenda kuamua mambo yao kama wanavyoona, wakipuuzia uzoefu na ushauri wa wakubwa wao. Tujiulize: Je, huu ndiyo uhuru tuutafutao? Katika mazingira kama haya kinachotafutwa si uhuru bali kuishi kwa kuheshimu vionjo binafsi. Ni muhimu sana kwa wanafamilia kuwa na uhuru wa pamoja katika kupanga na kuamua masuala kifamilia.

Tukijiruhusu kama wanajamii kuishi katika uholela upendo unatoweka. “Usikubali kitu chochote kuwa ni ukweli kama kinakosa upendo. Na usikubali kitu chochote kuwa ni upendo kama kinakosa ukweli! Hali moja bila nyingine ni uongo unaoharibu”. Kwa sababu “ni katika ukweli tu ndipo upendo inang’aa, ni katika ukweli tu ndipo tunapoweza kuuishi upendo kwa hakika."







All the contents on this site are copyrighted ©.