2014-03-13 11:42:51

TANZIA: Kardinali Josè Cruz Policarpo amefariki dunia


Kardinali Josè da Cruz Policarpo, Patriaki mstaafu wa Jimbo kuu la Lisbon, Ureno, amefariki dunia, Jumatano tarehe 12 Machi 2014 akiwa na umri wa miaka 78. Watu wengi ndani na nje ya Kanisa Katoliki wameguswa sana na msiba huu kwani ni kiongozi aliyeonesha imani kubwa, uvumilivu pamoja na kujitosa kimasomaso kwa ajili ya huduma kwa Mungu na jirani zake.

Kardinali Policarpo kwa miaka kumi na mitano alibahatika kuliongoza Jimbo kuu la Lisbon, yaani kuanzia mwaka 1998 hadi mwaka 2013. Mwenyeheri Yohane Paulo II akamteua na kumsimika kuwa Kardinali kunako Mwaka 2001. Kwa sasa Baraza la Makardinali linaundwa na Makardinali 217, kati yao kuna Makardinali 120 wenye haki ya kupiga na kupigiwa kura wakati wa mchakato wa uchaguzi wa Khalifa wa Mtakatifu Petro na wengine 97 waliobaki hawana tena haki ya kupiga wala kupigiwa kura.

Marehemu Kardinali Policarpo alizaliwa tarehe 26 Februari 1936 huko Alvorninha, Ureno. Akapadrishwa tarehe 15 Agosti 1961. Kuanzia Mwaka 1988 hadi mwaka 1996 alikuwa ni Mkuu wa Chuo Kikuu cha Kanisa Katoliki Ureno na ni mwandishi wa vitabu na makala mengi.

Tarehe 26 Mei 1978 aliteuliwa kuwa ni Askofu msaidizi wa Jimbo kuu la Lisbon, akawekwa wakfu tarehe 29 Juni 1978. Tarehe 5 Machi 1997 aliteuliwa na Mwenyeheri Yohane Paulo II kuwa Askofu mwandamizi wa Jimbo kuu la Lisbon na akamrithi Kardinali Antonio Ribeiro kama Patriaki wa Jimbo kuu la Lisbon hapo tarehe 24 Machi 1998. Alikuwa pia ni Mkuu wa Chuo Kikuu cha Ureno.

Mwaka 1999 hadi mwaka 2005 alikuwa ni Rais wa Baraza la Maaskofu Katoliki Ureno. Tarehe 3 Mei, 2011 alichaguliwa tena kuwa ni Rais wa Baraza la Maaskofu Katoliki Ureno. Tarehe 18 Mei 2013 akang'atuka kutoa madarakani kama Patriaki wa Jimbo kuu la Ureno.







All the contents on this site are copyrighted ©.