2014-03-13 11:43:45

Changamoto kwa waamini ni kuwa waaminifu kwa Kristo sanjari na kuchuchumilia utakatifu wa maisha!


Askofu Alvaro del Portilo alikuwa ni Padre mchapakazi aliyesimika maisha yake ya imani katika mwamba imara ambao ni Yesu Kristo. Ni ujumbe kutoka kwa Baba Mtakatifu Francisko ulioandikwa kwa niaba yake na Kardinali Pietro Parolin, Katibu mkuu wa Vatican, kwenda kwa washiriki wa Kongamano la Maadhimisho ya Kumbu kumbu ya Miaka 100 tangu alipozaliwa Askofu Portilo, Mkuu wa kwanza wa Chuo Kikuu cha Santa Croce, kilichoko mjini Roma, ambaye anatarajiwa kutangazwa kuwa ni Mwenyeheri hapo tarehe 27 Septemba 2014.

Askofu Portilo alijitahidi katika utume wake, kiasi kwamba, alibahatika kutembelea Mabara yote, huku akifuata nyayo za Mtakatifu Josemarìa. Ni mfano na kielelezo cha maisha yanayojikita katika unyenyekevu, uchangamfu na ukimya, lakini unaopania kuendeleza mwaliko wa kuchuchumilia utakatifu wa maisha na ushirikiano katika kazi ya kumkomboa mwanadamu.

Kongamano hili limefunguliwa, Jumatano, tarehe 12 Machi 2014 kwa hotuba ya utangulizi iliyotolewa na Askofu Javier Echevarrìa, Mkuu wa Chuo Kikuu cha Santa Croce na Mkuu wa Shirika la Kazi ya Mungu, maarufu kama Opus Dei. Anamshukuru Baba Mtakatifu Francisko anapofanya kumbu kumbu ya Mwaka mmoja tangu alipochaguliwa kuliongoza Kanisa Katoliki, changamoto kwa kila Mkristo kuhakikisha kwamba, anawatangazia wengine Injili ya Furaha kwa kuwashirikisha huruma na upendo wa Mungu usiokuwa na mipaka.

Papa Francisko ni mtu wa sala, aliyebahatika kuwa na kipaji cha kusikiliza kwa makini pamoja na kukutana na watu, sababu msingi ya kumshukuru Mungu kwa uwepo na utume wa Baba Mtakatifu Francisko. Anasema, Askofu Portilo kwa muda zaidi ya miaka arobaini alionesha uaminifu wake kwa Kristo na Kanisa lake pamoja na kwa Mtakatifu Josemarìa, mwanzilishi wa Shirika la Opus Dei.

Ni kiongozi aliyefaulu kumwilisha karama ya mwanzilishi wa Shirika la Opus Dei linaloundwa na Makleri pamoja na Waamini Walei na kwamba ni mfano bora wa kuigwa katika huduma kwa Mungu na jirani. Washiriki wa Kongamano hili wamekusanya fedha kwa ajili ya kugharimia miradi mbali mbali kwa Mwaka 2014 inayolenga kuwasaidia watu wa Nigeria kupata tiba; watoto wanaoishi nchini Pwani ya Pembe kupata huduma ya lishe bora pamoja na kuendeleza maboresho ya huduma ya afya Kinshasa, DRC.

Wajumbe wamechagia pia fedha kwa ajili ya kusaidia masomo kwa Mapadre kutoka Afrika wanaosoma kwenye Chuo Kikuu cha Kipapa cha Santa Croce, kilichoko mjini Roma. Kongamano hili linafungwa rasmi, Ijumaa tarehe 14 Machi 2014.







All the contents on this site are copyrighted ©.