2014-03-11 09:08:54

Watu wanatamani kuona Bara la Afrika limesimikwa katika amani ya kweli!


Shirikisho la Mabaraza ya Maaskofu Katoliki Afrika Magharibi, linaloundwa na Cape Verde, Guinea Bissau, Mauritania na Senegal katika ujumbe baada ya maadhimisho ya mkutano mkuu wa mwanzo wa Mwaka 2014 linawataka waamini na watu wote wenye mapenzi mema kuwa ni vyombo na wajenzi wa misingi ya haki na amani. Ni jukumu la kila mtu kufanya tafakari ya kina ili kung'amua umuhimu wa kusimama kidete kujenga, kulinda na kutetea haki na amani katika Jamii.

Maaskofu wanawataka waamini na watu wote wenye mapenzi mema kuwa ni mashahidi wa amani Barani Afrika kwa kuzingatia kwanza kabisa mafundisho yanayotolewa na Baba Mtakatifu Francisko kuhusu: ufukara, amani na mazingira. Waamini hawana budi kuwa ni wadau na wajenzi wa haki, amani na upatanisho, changamoto iliyotolewa na Mababa wa Awamu ya Pili ya Sinodi ya Maaskofu wa Afrika.

Waamini wanahimizwa kujisomea na kuutafakari ujumbe wa Baba Mtakatifu Francisko katika kipindi hiki cha Kwaresima, unaoongozwa na kauli mbiu "Maana mmejua neema ya Bwana wetu Yesu Kristo, jinsi alivyokuwa maskini kwa ajili yenu, ingawa alikuwa tajiri, ili kwamba, ninyi mpate kuwa matajiri kwa umaskini wake.

Maaskofu wanasema, ili haki, amani na upatanisho viweze kushamiri Barani Afrika, kuna haja ya kuwashirikisha wadau mbali mbali: viongozi wa Kanisa na Serikali; wanasiasa na wanaharakati ili kujikita daima katika njia ya majadiliano na amani ili kuweza kufikia malengo mbali mbali wanayojiwekea. Kwa wanasiasa wengi Barani Afrika, vita na kinzani za kijamii limekuwa ni suluhisho la migogoro na changamoto za maisha, jambo ambalo kwa sasa haliwezi kamwe kukubalika. Watu wajifunze kujadiliana na kutafuta suluhu ya migogoro kwa njia ya amani.

Maaskofu wanawahimiza waamini kuhakikisha kwamba, wanashiriki kikamilifu katika maadhimisho ya Liturujia na Ibada mbali mbali za Kanisa ili Mwenyezi Mungu aweze kuabudiwa na mwanadamu kutakatifuzwa. Familia za Kikristo zijenge na kuimarisha utamaduni wa kusali na kutafakari Neno la Mungu kwa pamoja, bila kusahau kumwombea Baba Mtakatifu Francisko katika maisha na utume wake.

Maaskofu wanasema kipindi cha Kwaresima ni muda muafaka uliokubalika kwa waamini: kufunga na kusali, kutafakari Neno la Mungu na kulimwilisha katika matendo adili. Kwaresima kiwe ni kipindi cha kuonjeshana upendo na mshikamano wa kidugu kwa njia ya huduma makini. Waamini wanapofunga na kujinyima, sadaka yao ilete mafao kwa maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii. Waamini waguswe na mahangaiko ya watu walioathirika kutokana na maafa asilia ndani na nje ya nchi zao, tayari kuwasaidia kwa hali na mali.







All the contents on this site are copyrighted ©.