Sala ya Baba yetu ni sala tuliyofundishwa na Kristo mwenyewe. Huu ni muhtasari wa
Mafundisho Makuu ya Yesu kwa wafuasi wake, kama yalivyo Mafundisho ya Heri za Mlimani
na Amri kuu ya Mapendo kwa Mungu na jirani. Mitume wa Yesu waliwaona wanafunzi wa
waalimu wengine wakifundishwa kusali na waalimu wao na ndipo wakamwomba Kristo wakisema
“Bwana utufundishe nasi kusali kama Yohane alivyowafundisha wanafunzi wake” (Lk 11:
1).
Kristo aliweka mbele yao sala hii yenye mistari mizito kabisa. Pengine
sote tu hodari katika kuisali sala hii. Kila siku katika ibada ya misa, katika sala
za familia na hata katika sala za jumuiya. Lakini nachelea kusema kuwa tunaweza kuwa
tumebaki katika kiwango cha kukariri tu sala hiyo bila kuona na kuonja uzito wa maneno
yake kiroho, bila kuona jinsi inavyopaswa kutuunganisha na kutuhusianisha na Mungu.
Katika
moja ya makanisa niliyobahatika kusali hapa mjini Roma nilikutana na maandishi fulani
ambayo nimeyaona kama yana chachu fulani katika kuitendetea haki sala ya Baba yetu
na hatimaye kuwa na tija katika maisha yangu kiroho. Maandishi hayo kwa ujumla yananikataza
kutamka kila neno la sala hii ya Baba yetu kama maisha yangu binafsi hayaakisi au
hayamaanishi maneno ninayotamka. Napenda kuwashirikisha maneno hayo kama yalivyoandikwa
na iwe fursa kwetu kutafakari vizuri uzuri na ukuu wa sala hii katika maisha ya kiroho.
•Usiseme
“Baba” wakati hujiweki mbele yake kama mwana
•Usiseme “yetu” wakati unaishi
katika ubinafsi wako
•Usiseme “uliye mbinguni” wakati daima unafikiri juu ya
mambo ya ulimwengu tu
• Usiseme “ufalme wako uje” wakati daima umechanganywa
na kupagaishwa na ufanisi wa malimwengu
•Usiseme “utakalo lifanyike duniani
kama mbinguni” wakati unakuwa mgunu kutokubali wakati mapenzi ya Mungu yanapokuwa
yanaumiza
• Usiseme “utupe leo mkate wetu wa kila siku” wakati hujali wengine
walio wahitaji na wanaoteseka kwa njaa
• Usiseme “utusamehe dhambi zetu” wakati
hauko katika hali ya kusamehe wengine
• Usiseme “usitutie kishawishini” wakati
bado tunaendelea kufanya dhambi
• Usiseme “utuopoe maovuni” wakati wewe mwenyewe
haupingani na uovu
• Na usiseme “amina” wakati huyatilii maanani mafundisho
ya sala ya Baba yetu
Tutafakari katika kipindi hiki cha Kwaresma japo maneno
haya na kuyaoanisha na maisha yetu ya kawaida kwani sala kama anavyosema Mtakatifu
Yohane Krisostomi “haifungwi na ratiba maalum tu bali ni hali inayodumu mchana na
usiku. Mtu anapaswa kumwuelekea Mungu sio tu pale anapomkumbuka kwa sala bali hata
anapokuwa anafanya mambo mengine” Sala ni maisha.
NAWATAKIENI KWARESMA
NJEMA. Padre Joseph Mosha. Jimbo kuu la Dar es Salaam.