2014-03-11 08:55:58

Jacques Maritaini mfuasi mkuu wa Yesu na mtetezi wa ukweli!


Taasisi ya Kimataifa ya Jacques Maritain inaadhimisha Miaka 40 tangu ilipoanzishwa na imekuwa na mchango mkubwa sana katika maisha na utume wa Kanisa na Jamii kwa ujumla. Ni Taasisi ambayo imejitahidi kumwilisha mawazo na mafundisho ya Mtakatifu Toma wa Akwino katika kutetea utu na heshima ya binadamu katika kazi ya uumbaji. Maritain alifanikiwa kutoa nyenzo muhimu katika kukabiliana na changamoto zilizokuwa zinajitokeza katika ulimwengu mamboleo.

Ni maneno yaliyosemwa hivi karibuni na Kardinali Pietro Parolin, Katibu mkuu wa Vatican katika maadhimisho ya Miaka 40 tangu Taasisi ya Kimataifa ya Jacques Maritaini ilipoanzishwa. Mafundisho yake yake yamewajengea watu uwezo wa kusimama kidete kulinda na kutetea utu na heshima ya binadamu; bila kutenganisha mahitaji ya mtu mzima: kiroho na kimwili. Akaonesha umuhimu wa utakatifu wa maisha, jambo msingi katika ulimwengu wa utandawazi.

Jacques Maritain katika baadhi ya kazi zake msingi anaonesha kwa kina na mapana kuhusu: Ukristo na Demokrasia, jambo ambalo limelisaidia mchakato wa Kanisa kujihusisha na masuala ya kidemokrasia. Alizungumzia kuhusu haki msingi za binadamu na sheria asilia; mambo ambayo aliyaandika mara tu baada ya vita kuu ya Pili ya Dunia, alipokuwa uhamishoni huko Manhattan, ambako wafungwa wengi kutoka Barani Ulaya, walimwona kuwa ni kiongozi wa maisha ya kiroho.

Aliandika kitabu kinachoonesha uhusiano kati ya mtu na serikali; mambo yanayoonesha mabadiliko makubwa yaliyojitokeza huko Ufaransa na Marekani, kuhusiana na haki msingi za binadamu mintarafu mtazamo wa Kanisa. Huyu ni kati ya wasomi waliotayarisha mazungumzo kuhusu Tamko la Haki Msingi za Binadamu kunako mwaka 1948. Kazi zote hizi anasema Kardinali Parolin zimekuwa ni msaada mkubwa katika maandalizi ya Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican.

Kutokana na mchango wote huu, Kardinali Parolin ameipongeza Taasisi ya Kimataifa ya Jacque Maritain kwa mchango wake katika maisha na utume wa Kanisa na Jamii katika ujumla wake. Taasisi hii inaendelea kujadiliana na mabingwa katika Falsafa ili kuhuisha mchango wa Jacque Maritain kwa kusoma alama za nyakati katika Karne ya ishirini na moja.

Kanisa linaendelea kuonesha matumaini yake ya dhati katika mchango unaotolewa na Taaisi hii kwa sasa na kwa siku za usoni. Kanisa linamshukuru Jacques Maritain kwa mawazo na ushuhuda wake katika mchakato wa kuyatakatifuza malimwengu. Kwa hakika anasema Kardinali Pietro Parolin, Jacques Maritain ni mfuasi mkubwa wa Yesu na mtetezi wa ukweli.







All the contents on this site are copyrighted ©.