2014-03-10 12:01:22

Yesu Kristo ni kiini cha imani ya Kanisa


Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto wa kumi na sita, amemwandikia ujumbe wa pongezi na shukrani Professa Achim Buckenmaier mratibu wa Kongamano la Kimataifa linalonyika kwenye Chuo Kikuu cha Jordan, Jimbo Katoliki Morogoro, Tanzania, ili kujifunza kwa kina na mapana taalimungu kuhusu Yesu wa Nazareti, kama inavyochambuliwa na Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto XVI.

Hili kongamano la pili kufanyika Barani Afrika, baada ya kongamano la kwanza kufanyika nchini Benin, Septemba 2013. Kongamano hili linaongozwa na kauli mbiu " Wewe unatoka wapi?.

Lengo ni kuwajengea uwezo wanafunzi wa vyuo vikuu Barani Afrika, kutambua taalimungu ya Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto wa kumi na sita, kwa kuondoa vizingiti vinavyokwamisha watu kufahamu utajiri mkubwa unaofumbatwa katika vitabu vilivyoandikwa na Papa mstaafu Benedikto wa kumi na sita. Kongamano hili limefunguliwa Jumatatu, tarehe 10 na linatarajiwa kuhitimishwa tarehe 12 Machi 2014. Linahudhuriwa na Maaskofu, Mapadre, watawa na waamini walei kutoka ndani na nje ya Tanzania.

Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto XVI anasema, Yesu Kristo ni kiini cha imani ya Kanisa, kumbe kukutana naye kunamwezesha mwamini kuweza kukutana pia na Mwenyezi Mungu aliye hai. Hii ni changamoto kubwa kwa Mama Kanisa kwani leo hii kuna upinzani juu ya uelewa wa Yesu wa Nazareti, jambo ambalo limemsukuma kuandika vitabu juu ya Yesu wa Nazareti, ili kutoa nafasi kwa Waamini na watu wenye mapenzi mema kumkaribia na hatimaye, kumfahamu Kristo.

Ni matumaini ya Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto wa kumi na sita kwamba, Kongamano hili la kimataifa litawawezesha washiriki kukutana na hatimaye kutoka kifua mbele kutangaza kwa nguvu na moyo mkuu Injili na kwamba, Yesu ni chemchemi ya maji ya uzima.







All the contents on this site are copyrighted ©.