2014-03-10 08:16:16

Papa yuko Jangwani ili kufunga na kusali


Baba Mtakatifu Francisko pamoja na wasadizi wake wa karibu, Jumapili jioni waliondoka wote kwa Mabus mawili kuelekea mjini Arricia, nje kidogo ya Roma kwa ajili ya mafungo ya maisha ya kiroho, kama sehemu ya mchakato wa kujitakasa. Mafungo haya yanaongozwa na Monsinyo Angelo de Donatis, Paroko wa Parokia ya Mtakatifu Marko, Jimbo kuu la Roma. RealAudioMP3

Hiki ni kipindi cha kufunga ili kuzuia vilema vya kibinadamu, tayari kuinua mioyo ili kuomba neema na nguvu katika utekelezaji wa majukumu yao ya kila siku. Hiki ni kipindi cha kujinyima ili kuwaondolea kiburi kwa kutambua kwamba, kama binadamu wanaweza kuogelea katika dhambi, hivyo wanahitaji kujipatanisha na Mungu pamoja na jirani zao.

Mafungo haya yameanza rasmi, Jumapili tarehe 9 Machi na yanatarajiwa kukamilika Ijumaa tarehe 14 asubuhi. Hii ni nafasi maalum kwa Baba Mtakatifu Francisko kuweza kufanya tafakari ya kina, mwaka mmojua tangu alipoteuliwa kuliongoza Kanisa Katoliki, hapo tarehe 13 Machi 2014. Mafungo haya yanasheheni: Ibada ya Fumbo la Ekaristi Takatifu, Tafakari pamoja na Ibada ya Kuabudu Ekaristi Takatifu; mambo msingi katika mafungo.

Papa Paulo wa sita, aliwahi kusema kwamba, mafungo ya maisha ya kiroho kwa Wakatoliki yanakwenda sanjari na Sakramenti ya Upatanisho kwa Mungu na jirani, kama njia ya kujipatia neema na baraka kutoka kwa Mwenyezi Mungu, ili kusaidia kuwaongoza watu wake wanaopambana na ubinadamu ulioathiriwa kutokana na dhambi ya asili; ni jitihada za kuomba huruma ya Mungu ili aweze kuponya madonda ya ubinadamu pamoja na kuimarisha malengo na matumaini ya watoto wake siku kwa siku.

Mafungo yanawasaidia waamini kuwa na moyo mpya unaojikita katika neema na baraka kutoka kwa Mwenyezi Mungu, ili kushinda vilema na udhaifu wa kibinadamu. Waamini wanaalikwa na Mama Kanisa kuhakikisha kwamba, kila wakati wanachunguza dhamiri zao mbele ya Mwenyezi Mungu, ili kushukuru, kusifu na kumwabudu Mwenyezi Mungu mwingi wa huruma na mapendo.

Ni wakati wa kuchunguza ahadi ambazo mwamini ameziweka mbele ya Mungu na jirani zake, ili kuangalia kama kweli amejitahidi kuzitekeleza au amekwama. Mafungo ya kiroho, yawe ni fursa kwa waamini kuthamini utendaji wa majukumu yao kwa Mungu na mbele ya Jamii; wawe tayari kubadilisha na kujipanga upya kwa mambo ambayo hayaendi kwa kuamini kwamba, bado kuna uwezekano wa kutenda vizuri zaidi badala ya mtu kujikatia tamaa.

Baba Mtakatifu Francisko katika mahojiano maalum na Gazeti la “Corriere della Sera” linalochapishwa kila siku nchini Italia. Anasema, alipokuja mjini Roma kushiriki katika mkutano wa Baraza la Makardinali kwa ajili ya uchaguzi wa Khalifa wa Mtakatifu Petro, hakuwa na wazo kwamba, angeweza kuchaguliwa na hivyo kulazimika kuhama kutoka Argentina hadi mjini Vatican.

Anasema ameanza kutekeleza utume wake wa kuliongoza Kanisa Katoliki kwa kutekeleza kwanza kabisa ushauri uliokuwa umetolewa na Makardinali katika vikao vyao elekezi kabla ya uchaguzi wa Khalifa wa Mtakatifu Petro. Ameendelea kumtegemea Mwenyezi Mungu katika utendaji wa shughuli zake za kichungaji.

Baba Mtakatifu anasema, kati ya mambo msingi yaliyokaziwa na Makardinali ni huduma ya maisha ya kiroho kwa wasaidizi wake wa karibu waliopewa dhamana katika kusimamia na kuongoza Mabaraza ya Kipapa na Taasisi mbali mbali zinazomwezesha kutekeleza utume wake kama Khalifa wa Mtakatifu Petro.

Jambo la kwanza ni kuhakikisha kwamba, kila mwezi wanapata fursa ya kujitenga na shughuli za kila siku, ili kufanya mafungo ya maisha ya kiroho. Kila mtu anayo haki ya kupata siku tano za mafungo ya kiroho. Mafungo ya Kipindi cha Kwaresima kwa wakati huu ni mwendelezo wa utekelezaji wa maazimio ya Mikutano Elekezi ya Makardinali iliyofanyika kabla ya uchaguzi wa Khalifa wa Mtakatifu Petro.

Baba Mtakatifu anasema katika mahojiano hayo kwamba, Mafungo ya maisha ya kiroho yanamwezesha mwamini kujitenga na marafiki, mazingira na shughuli za kawaida, ili kuweza kupata muda wa kusali, kutafakari na kufanya maamuzi ya kina katika maisha na utume wa Kanisa. Mafungo yana faida kubwa zifuatazo: kwanza kabisa yanamwezesha mwamini kupata muda zaidi wa kumshuruku, kumsifu na kumtukuza Mwenyezi Mungu pamoja na kuendelea kujifunza kwa njia ya ukimya kutoka kwake.

Pili ni nafasi ya kutuliza mawazo, ili hatimaye, kujenga na kuimarisha utashi wa kupenda kumtumikia Mwenyezi Mungu kwa moyo na akili zako zote. Tatu katika mazingira ya upweke chanya, mwamini anapata nafasi kubwa zaidi ya kushikamana na Mwenyezi Mungu pamoja na Yesu Kristo, ili kujichotea neema na nguvu ya kutekeleza nyajibu mbali mbali katika maisha na utume wa Kanisa.







All the contents on this site are copyrighted ©.