Papa Francisko kutembelea Korea ya Kusini, kuanzia tarehe 14-18 Agosti 2014
Taarifa kutoka Vatican zinabainisha kwamba, Baba Mtakatifu Francisko amepokea kwa
moyo mkuu mwaliko uliotolewa na Rais wa Jamhuri ya Watu wa Korea pamoja na Baraza
la Maaskofu Katoliki nchini humo kutembelea Korea na kushiriki katika Maadhimisho
ya Siku ya Sita ya Vijana wa Asia, itakayoadhimishwa Jimboni Daejeon, Korea ya Kusini.
Maadhimisho haya taanza kutimua vumbi kuanzia tarehe 14 hadi tarehe 18 Agosti
2014. Hii itakuwa ni hija ya kwanza ya kitume kufanywa na Baba Mtakatifu Francisko
Barani Asia, tangu alipochaguliwa kuliongoza Kanisa Katoliki, Mwaka mmoja uliopita.
Hayo yamebainishwa na Padre Federico Lombardi, msemaji mkuu wa Vatican alipokuwa
anazungumza na waandishi wa habari mjini Vatican siku ya Jumatatu, tarehe 10 Machi
2014.