2014-03-10 14:58:17

Hija ya Papa Francisko nchini Korea ilete matumaini ya upatanisho wa kweli!


Kardinali Andrew Yeom Soo-jung, Askofu mkuu wa Jimbo kuu la Seoul, Korea ya Kusini, amepokea taarifa rasmi ya hija ya kitume itakayofanywa na Baba Mtakatifu Francisko nchini humo kama sehemu ya Maadhimisho ya Siku ya sita ya Vijana Barani Asia kwa moyo mkuu na wa shukrani.

Anapenda kuchukua fursa tangu wakati huu kumkaribisha Baba Mtakatifu nchini Korea kwa mikono miwili, ili kuweza kukutana, kuzungumza na kusali na vijana kutoka Barani Asia, watakaokuwa wanakusanyika kwenye Jimbo Katoliki la Dejeon, bila kuwasahau waamini na watu wenye mapenzi mema wanaoendelea kuonesha hamu ya kukutana na Baba Mtakatifu Francisko.

Kardinali Yeom Soo-jung anasema, wakati wa Ibada ya Misa ya shukrani baada ya kusimikwa kuwa Makardinali, Baba Mtakatifu alimshirikisha upendo wake mkuu kwa wananchi wa Korea na kwamba, sasa ameamua kufanya hija ya kitume nchini mwao, jambo ambalo linaonesha neema na baraka kutoka kwa Mwenyezi Mungu kwa ajili ya wananchi wa Korea.

Ni matumaini ya wananchi wa Korea kwamba, hija ya Baba Mtakatifu itasaidia kukoleza mchakato wa upatanisho kati ya Korea ya Kusini na Kaskazini sanjari na Bara zima la Asia kusikia dhamana ya kulinda na kujenga amani, upendo na mshikamano kati ya watu.

Hija hii iwe ni fursa kwa maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii kuwa na matumaini mapya katika maisha na vipaumbele vyao.







All the contents on this site are copyrighted ©.