2014-03-08 11:39:17

Yaliyojiri katika mazungumzo kati ya Katibu mkuu wa Baraza la Makanisa Ulimwenguni na Papa Francisko


Dr. Olav Fykse Tveit, Katibu mkuu wa Baraza la Makanisa Ulimwenguni, Ijumaa tarehe 7 Machi 2014 amekutana na kuzungumza na Baba Mtakatifu Francisko mjini Vatican. Katika mazungumzo yake na Baba Mtakatifu Dr. Tveit amekazia umuhimu wa kukuza na kudumisha majadiliano ya kiekumene miongoni mwa Wakristo ili kujenga na kudumisha umoja. RealAudioMP3

Dr Tveit amempongeza Baba Mtakatifu Francisko kwa juhudi zake katika kuombea amani nchini Syria, changamoto na mwaliko kwa Makanisa kusimama kidete kujenga uchumi unaojimbanua katika misingi ya haki. Itakumbukwa kwamba, Baraza la Makanisa Ulimwenguni lina jumla ya Makanisa wanachama 345 yaliyoenea katika nchi zaidi ya 110.

Katibu mkuu wa Baraza la Makanisa Ulimwenguni alikuwa mjini Vatican kwa mwaliko wa Baraza la Kipapa linalohamasisha Umoja wa Wakristo. Anakiri kwamba, katika mapambazuko ya Millenia ya tatu ya Ukristo, Mwenyezi Mungu anaendelea kufungua njia za majadiliano ya kiekumene, ili kwa pamoja Wakristo waweze kushuhudia imani yao kwa Kristo na Kanisa lake kwa njia ya huduma makini hasa zaidi miongoni mwa wale wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii kutokana na hali yao ya maisha. Wakristo wahamasishwa na Baba Mtakatifu Francisko kushikamana ili kuweza kuwatangazia Watu wa Mataifa, Injili ya Furaha.

Kwa upande wake, Katibu mkuu wa Baraza la Makanisa Ulimwenguni anasema, amefurahishwa kwa namna ya pekee na mwaliko na changamoto inayotolewa na Baba Mtakatifu Francisko katika mshikamano na ushuhhuda wa ujenzi wa misingi ya haki, amani na upendo kati ya Wakristo na Walimwenguni katika ujumla wao. Injili inapaswa kupewa kipaumbele cha kwanza kwa Wakristo.

Dr. Tveit amezungumzia Nyaraka mbali mbali zilizokwishawahi kutolewa na Baraza la Makanisa Ulimwenguni, kwa kukazia umuhimu wa Kanisa kuwa ni mhudumu; Kanisa ambalo linapaswa kuwa ni nyumba ya wote, ili kuwashirikisha wengine wote Habari Njema ya Wokovu.

Dr. Tveit amezungumzia kuhusu hija ya kichungaji itakayofanywa na Baba Mtakatifu Francisko kwenye Nchi Takatifu, ili kukutana, kusali na kuzungumza na Patriaki Bartolomeo wa kwanza wa Costantinopoli. Amempongeza Baba Mtakatifu kwa ujasiri wake unaoonesha jinsi ambavyo anakereketwa na ukosefu wa amani na utulivu huko Mashariki ya Kati.

Ni matumaini ya Baraza la Makanisa Ulimwenguni kwamba, hija hii ya kichungaji ya Baba Mtakatifu itasaidia kukoleza mchakato wa amani, utulivu na upatanisho huko Mashariki ya Kati. Kwa miaka mingi Baraza la Makanisa Ulimwenguni limesali na kujielekeza katika ujenzi wa misingi ya haki na amani huko Nchi Takatifu.

Dr. Olav Fykse Tveit anakazia kwamba, dini na imani vina mchango mkubwa katika ustawi, maendeleo na mafao ya wengi. Haki, amani na upatanisho ni mambo yanayowezekana kwani ni tunu msingi za maisha ya dini mbali mbali duniani. Israeli na Palestina ni nchi mbili zinazoweza kuishi kwa amani na utulivu kwa kuheshimiana.

Baraza la Makanisa Ulimwenguni linaendelea kuwahamasisha waamini na watu wote wenye mapenzi mema kujikita katika hija ya haki na amani, changamoto kubwa iliyotolewa na wajumbe wa mkutano mkuu wa Baraza la Makanisa Ulimwenguni uliohitimishwa kunako Mwaka 2013 huko Busan, Korea ya Kusini. Mabadiliko ya tabia nchi ni kati ya masuala ambayo pia yanapaswa kufanyiwa kazi na Wakristo katika umoja wao, sanjari na ujenzi wa mkakati wa uchumi wa haki. Ikiwa kama tunu hizi msingi zitashindwa kumwilishwa katika vipaumbele vya mwanadamu, watakaoendelea kuumia ni maskini wanaoishi katika nchi maskini zaidi duniani.

Baraza la Makanisa Ulimwenguni linawaalika wadau mbali mbali kuhakikisha kwamba, wanaibua mbinu mkakati wa kulinda na kutunza mazingira. Dr. Tveit anasema, ameridhika sana na mazungumzo aliyofanya na Baba Mtakatifu Francisko wakati wa hija yake ya kichungaji mjini Vatican.







All the contents on this site are copyrighted ©.