2014-03-08 10:43:28

Rais wa Baraza la Kipapa la haki na amani kutembelea Sudan ya Kusini


Kardinali Peter Turkson, Rais wa Baraza la Kipapa la Haki na Amani anatarajiwa kufanya hija ya kichungaji nchini Sudan ya Kusini kuanzia tarehe 18 Machi hadi tarehe 23 Machi 2014 kama kielelezo cha mshikamano wa upendo kutoka kwa Baba Mtakatifu Francisko kwa wananchi wa Sudan ya Kusini wanaokabiliwa na maafa makubwa kwa sasa.

Taarifa kutoka katika Idara ya Habari ya Shirikisho la Maaskofu Afrika Mashariki na Kati, AMECEA inaonesha kwamba, habari hizi zimetolewa na Askofu mkuu Paolino Lukudu Loro wa Jimbo kuu la Juba, Sudan ya Kusini. Akiwa nchini humo, Kardinli Turkson ataadhimisha Ibada ya Misa Takatifu pamoja na kutabaruku Kanisa la Parokia ya Mtakatifu Yosefu, Jimbo kuu la Juba. Ratiba elekezi inaonesha kwamba, tukio hili linatarajiwa kufanyika hapo tarehe 19 Machi 2014.

Alhamisi tarehe 20 Machi, Kardinali Turkson anatarajiwa kukutana na kuzungumza na Taifa la Mungu nchini Sudan ya Kusini. Ijumaa tarehe 21 Machi atakutana na kuzungumza na Rais Salva Kiir Mayardit pamoja na viongozi wengine wa Makanisa nchini Sudan ya Kusini.

Hija hii ya kichungaji inayofanywa na Kardinali Turkson nchini Sudan ya Kusini, itakamilika kwa Ibada ya Misa Takatifu itakayoadhimishwa kwenye Kanisa kuu la Mtakatifu Theresa, Kator na baadaye, Jumatatu, tarehe 23 Machi, Kardinali Turkson atarejea mjini Vatican kuendelea na shughuli zake za kichungaji.







All the contents on this site are copyrighted ©.