Elimu kwa vijana wa kizazi kipya ipewe kipaumbele cha kwanza!
Mke wa Waziri mkuu wa Tanzania, Mama Tunu Pinda amewataka wazazi hapa nchini watoe
kipaumbele kwenye suala la elimu kwa vijana bila ubaguzi wa kijinsia. Ametoa wito
huo Jumamosi, Machi 8, 2014 wakati akifungua Kongamano la Wanawake wa Afrika ikiwa
ni sehemu ya kuadhimisha Siku ya Wanawake Duniani lililofanyika kwenye ukumbi wa Karimjee,
Jijini Dar es Salaam.
Kongamano hilo liliandaliwa na Chama cha Walimu Wanawake
Tanzania (Tanzania Women Teachers’ Association - TAWOTEA) kwa kushirikiana na taasisi
ya African Women Charity Organisation ya Oakland, California, Marekani.
Akizungumza
na washiriki wa kongamano hilo, Mama Tunu Pinda alisema: ”Ninawaomba wazazi wenzangu,
wake kwa waume tuungane kwa pamoja kwa kutoa kipaumbele kwenye suala zima la elimu
kwa vijana wetu bila ubaguzi wa kijinsia. Kwa kufanya hivyo tutawajenga wavulana na
wasichana ili wawe na uwezo wa kiuchumi na uthubutu katika masuala ya uongozi na maisha
yao ya baadaye.” Akizindua mfuko wa elimu ulioanzishwa na chama hicho, Mama Pinda
alisema ana imani utakuwa endelevu na utakidhi malengo ya kuazishwa kwake ambayo ni
kuwasaidia watoto wenye uhitaji na waishio kwenye mazingira ili wapate elimu ya msingi
na ya sekondari.
”Mkiwa ni waalimu wanawake na tena ni walezi wa watoto wetu,
mmefanya jambo kubwa na la kihistoria kwa kuanzisha mfuko wa elimu mlioamua kuuita
Tanzania Education Fund (TEF). Nimedokezwa kwamba malengo ya mfuko huu ni kusaidia
gharama za elimu ya msingi na sekondari kwa watoto wa kike na wa kiume na hasa kwa
watoto walio kwenye mazingira magumu na wenye uhitaji. Ni matumaini yangu kwamba utakuwa
endelevu.”
”Ni imani yangu kwamba kupitia mfuko huu unaozinduliwa rasmi leo
hii, utaowaongezea vijana wetu wa kike na wa kiume wigo wa kupata elimu ambapo kama
mfuko huu usingekuwepo, isingekuwa rahisi kwao kumudu gharama za masomo,” aliongeza.
Aliwaomba wadau wote wa elimu na wananchi kwa ujumla, waunge mkono juhudi za walimu
hao katika kuikomboa nchi hii, hasa katika sekta ya elimu huku wakiamini elimu ni
ufunguo wa maisha.
Mapema, akisoma risala yao, Mkurugenzi Mtendaji wa TAWOTEA,
Mwl. Neema Kabale alisema asasi hiyo ambayo imesajiliwa tangu mwaka 2008, inajihusisha
na utetezi wa haki za msingi za wanawake, wasichana, vijana na watoto katika masuala
ya elimu, afya, na upatikanaji wa chakula. Katika kongamano hilo la siku moja, asasi
hiyo iliandaa mada sita zikiwemo za “Ushiriki wa wanaume katika ukombozi wa mwanamke”
na “Majukumu ya Vijana katika Muungano wa Afrika”.
Akitoa hitoria fupi ya Kongamano
la Wanawake Afrika, Rais wa taasisi ya African Women Charity Organisation ya Oakland,
Marekani, Bi. Rwanda Saleem, alisema Tanzania ni nchi ya nane kupata fursa ya kuratibu
wa kongamano kama hili. ”Barani Afrika tayari nchi saba zimekuwa waratibu wa kongamano
hili ambazo ni Ghana, Guinea, Gambia, Senegal, Kenya, Rwanda, na Msumbiji ambayo ilikuwa
mwenyeji mwaka jana. Tanzania imepewa fursa ya kuandaa kongamano hili mwaka huu,”
aliongeza.
Kaulimbiu ya kongamano hilo ni “Kujenga Muungano wa Afrika kwa
Kushirikisha Wanawake kwenye Uongozi” (The Unification of Africa Through the Emancipation
of Leadership of Women).