2014-03-08 08:03:13

Dhamana na wajibu wa Mashirika ya Kitawa na Kazi za kitume ndani ya Kanisa


Hivi karibuni Baba Mtakatifu Francisko alikutana na kuzungumza na Wakuu wa Mashirika ya Kitawa na Kazi za Kitume Kimataifa waliokuwa wamehitimisha maadhimisho ya mkutano mkuu wa 82 uliofanyika mjini Roma. RealAudioMP3

Ni mkutano uliojikita katika majadiliano ya kina kati ya Baba Mtakatifu na Wakuu wa Mashirika katika hali ya kidugu, kwa kutambua kwamba, watawa kama sehemu ya binadamu wengine wote ni Wadhambi na Manabii katika ulimwengu mamboleo.

Baba Mtakatifu akizungumzia kuhusu utambulisho na utume wa watawa anasema, wanapaswa kuishi maisha yanayotoa ushuhuda wenye mvuto na mashiko unaojikita katika maisha ya kujisadaka; upendo na ukarimu kwa jirani, lakini zaidi kwa maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii. Watawa wawe makini ili wasije wakamezwa na malimwengu kwani hapa watalichefua Kanisa!

Ushuhuda adili na amini wa maisha ya kitawa na kazi za kitume ulete harufu nzuri yenye mvuto kwa watu kulipenda na kulithamini Kanisa; kwa kujitosa kinaganaga kuleta mabadiliko yanayokusudiwa na Mama Kanisa katika ulimwengu mamboleo. Ili kufanikisha azma hii, watawa hawana budi kwanza kabisa: kujikita katika maisha na tunu msingi za Kiinjili, ingawa huu ni mwaliko na changamoto kwa Familia yote ya Mungu.

Watawa wawe ni watu safi, wakweli na wa wazi kwa kutambua kwamba, ulimwenguni kuna uwepo wa neema na dhambi. Hakuna mtu mkamilifu hapa duniani, kila mtu ana kasoro na mapungufu yake na hii ni sehemu ya ubinadamu. Kwa kutambua kasoro na karama zao, watawa wanaweza kujitosa kifua mbele kushuhudia Kweli za Kiinjili bila ya kuwa na makunyanzi.

Baba Mtakatifu Francisko anawaalika watawa kuondokana na misimamo mikali ya maisha ya kitawa na badala yake wawe ni njia na mwanga kwa siku za usoni. Watawa wawe tayari kujifunza mahangaiko ya maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii, ili waweze kuwashirikisha upendo na huruma ya Mungu inayobubujika kutoka kwa Kristo na Kanisa lake. Watawa wajikite katika maisha ya Sala na Tafakari ya kina ya Neno la Mungu, tayari kuwaonjesha jirani zao Injili ya Furaha.

Baba Mtakatifu anasema kipaumbele cha kwanza kwa Watawa katika Mapambazuko ya Millenia ya tatu ya Ukristo ni kuhakikisha kwamba, wanajitosa kimasomaso kutangaza Habari Njema ya Wokovu sanjari na kushiriki katika mchakato wa ujenzi wa Ufalme wa Mungu duniani kama walivyofanya watawa wengi katika utume na maisha ya Kanisa. Watawa wawe waaminifu kwa karama za Mashirika yao; wajitahidi kuwa wagunduzi na tayari kusoma alama za nyakati kama wanavyokazia Mababa wa Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican.

Baba Mtakatifu anasema, takwimu zinaonesha kwamba, kuna idadi kubwa ya miito ya kitawa Barani Asia na Afrika, jambo linalotoa changamoto nyingi katika mchakato wa utamadunisho wa karama za Mashirika ya Kitawa na Kazi za Kitume. Mashirika yanapaswa kuwa makini katika uteuzi wa vijana wanaoomba kujiunga na mashirika yao. Waangalie na kukoleza majadiliano ya kidini sanjari na kuangalia uwakilishi wa Mashirika ya Kitawa katika taasisi zinazoongozwa na kusimamiwa na Serikali mbali mbali.

Baba Mtakatifu anawahimiza watawa wasihofu kukufanya makosa katika kumwilisha karama ya mashirika yao kwani hii ni sehemu ya ubinadamu; jambo la msingi ni kuomba msamaha tayari kurekebisha mapungufu yaliyojitokeza ili kusonga mbele kwa imani na matumaini zaidi. Vijana wanaoomba kujiunga na maisha ya kitawa hawana budi kulelewa vyema kwa kuangalia tamaduni na mazingira ya watu husika, tayari kutamadunisha karama ya shirika husika. Hapa watawa watambue kwamba, utamadunisho wa karama ni jambo muhimu sana katika maisha na ustawi wa Mashirika husika.

Baba Mtakatifu ameonya kuhusiana na biashara haramu ya binadamu inayoweza kufanywa na Mashirika ya Kitawa yanayotafuta vijana wa kujiunga na mashirika haya kwa udi na uvumba kutoka katika Nchi changa zaidi duniani na kuwapeleka Ulaya. Onyo hili liliwahi kutolewa na Maaskofu kutoka Ufilippini wakati wa Maadhimisho ya Sinodi ya Maisha ya Kuwekwa wakfu iliyoadhimishwa kunako Mwaka 1994.

Baba Mtakatifu anasikitika kusema kwamba, wito wa “Ubruda” bado haujafahamika na kupokelewa kwa moyo chanya na waamini wengi. Hii ndiyo maana wito huu unaendelea kufifia siku hadi siku ndani ya Kanisa. Baraza la Kipapa la Mashirika ya Kitawa na Kazi za Kitume, lilipewa dhamana ya kuangalia kwa kina na mapana changamoto zinazojitokeza katika maisha ya kitawa; wajitahidi kusoma alama za nyakati na kujitahidi kufahamu Mwenyezi Mungu anataka nini kwa Kanisa?

Baba Mtakatifu Francisko anasema malezi ni jambo la muhimu sana, linalohitaji: hekima na busara; upendo na subira; sala na bidii. Ikumbukwe kwamba, nyumba za malezi si “Kituo cha Polisi”. Vijana wenye nia ya kutaka kuwa watawa hawana budi kufundwa: Kiroho, kiakili na kiutu; Maisha ya Kijumuiya na kazi za kitume; utamadunisho na majadiliano yanayojikita katika ukweli na uwazi na kwamba, unafiki ni sumu ya maisha ya kitawa. Vijana wapewe fursa na kusaidiwa kutafakari kuhusu maisha na wito wao, ili hatimaye, waweze kutoa uamuzi wenye busara.

Watu wa Mungu wajengewe ukomavu na uhuru katika maisha yao ya Kikristo. Seminari na nyumba za malezi, ziwe ni jukwaa la majadiliano ya kina, ukweli na uwazi bila woga. Walezi wajitahidi kufahamu lugha inayotumiwa na vijana ili waweze kuwasiliana vyema zaidi kutoka katika undani wa mioyo yao na wala si katika hali ya kujisikia tu! Malezi yalenge ukomavu wa mtu mzima na hatima ya maisha yake. Lengo ni kuhakikisha kwamba, watawa wanakuwa kweli ni mashahidi wa Kristo Mfufuka. Vijana watambue kwamba, wanaandaliwa kuwa ni viongozi wakuu wa Familia ya Mungu na wala si mameneja katika kampuni Fulani.

Baba Mtakatifu Francisko anasema kwamba, kuna changamoto kubwa katika malezi, yaani tatizo la kumpokea Mseminari aliyefukuzwa kutoka Shirika au Jimbo Fulani na kumpatia tena nafasi ya kuendelea na majiundo yake ya maisha ya kitawa. Kanisa linatambua kwamba, watoto wake si wakamilifu, ni wadhambi, lakini Kanisa haliwezi kukubali watoto wake wawe mafisadi! Hii inaonesha kwamba, malezi yanakabiliwa na changamoto nyingi, hasa baada ya kuibuka kashfa za nyanyaso za kijinsia dhidi ya watoto wadogo ndani ya Kanisa.

Watawa wanapaswa kujifunza kuishi kwa pamoja kama ndugu katika Kristo kwa kujitahidi kufisha ubinafsi na kasoro zao ili kuondokana na kinzani pamoja na migogoro isiyokuwa ya lazima. Masilahi ya Jumuiya hayana budi kupewa kipaumbele cha kwanza, kwani maisha na mshikamano wa Kijumuiya una nguvu ya kujenga na kudumisha umoja, upendo, mshikamano na utume.

Kinzani na misigano ni mambo ya kawaida katika maisha ya mwanadamu. Mambo haya yanapojitokeza, yajadiliwe kwa kina na mapana kwa kuzingatia: upendo, ukweli na uwazi, tayari kuendeleza umoja na mshikamano wa Jumuiya. Watawa watambue kwamba, umoja ni nguvu na utengano ni udhaifu. Pale kinzani zinapojitokeza, wanajumuiya watafute ushauri wa kiroho, wakijikita katika upole na unyenyekevu, ili kuganga misigano hii inayoweza kuacha madonda makubwa katika maisha ya watawa!

Baba Mtakatifu anakemea ukatili unaofanywa kwenye Mashirika ya kitawa na kazi za kitume, kwani hii ni sumu kali dhidi ya maisha ya Kijumuiya. Watawa wasijitafute wenyewe na mafao yao binafsi, daima wajitahidi kuongozwa na moyo mnyofu! Udugu na umoja katika maisha ya kitawa ni jambo nyeti linalohitaji moyo wa mtu kujisadaka katika Fumbo la Ekaristi Takatifu ili kuona na kutambua ukweli wa mambo!

Baba Mtakatifu akizungumzia kuhusu uhusiano kati ya Mashirika ya Kitawa na Makanisa mahalia anasema, Waraka wa kichungaji uliochapishwa kunako Mwaka 1978 kuhusu uhusiano kati ya Watawa na Maaskofu bado ni muhimu sana na wala haujapitwa na wakati. Watawa wanapaswa kujenga uhusiano wa dhati na Makanisa mahalia, ili kulinda na kuendeleza karama za Mashirika haya katika Makanisa mahalia. Karama hizi ziheshimiwe na kuthaminiwa katika maisha na utume wa Makanisa mahalia.

Maaskofu watambue kwamba, Watawa ni wadau wa Uinjilishaji; watu wenye karama na utajiri mkubwa katika utume na maisha ya Makanisa mahalia. Maaskofu na watawa wajenge utamaduni wa mawasiliano. Kuna haja kwa Maaskofu na Watawa kupitia uhusiano wao ili kurekebisha kasoro zilizojitokeza, kwa kutambua kwamba, watawa ni wadau muhimu sana katika Unjilishaji Mpya. Hawa ni watu wanaojitoa kwa hali nam ali kwa ajili ya huduma kwa: Maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii; katika sekta ya elimu, afya na maendeleo endelevu. Katika huduma kwa maskini, Baba Mtakatifu anasema, huko wapelekwe watawa wenye sifa, ari ya kuhudumia; watu wa Sala na tafakari ya Neno la Mungu, kumbe haitoshi kuwa mtawa tu!

Baba Mtakatifu Francisko anatambua fika umuhimu wa sekta ya elimu kwani hapan i mahali pa kurithisha tunu msingi za maisha ya kiutu na kiimani; ni mahali muafaka pa kutangazia Injili ya Kristo. Watawa wawe makini katika majiundo ya wanafunzi wanaohudhuria masomo kwenye taasisi zao kwani kuna changamoto nyingi katika maisha ya ndoa na familia; mambo ambayo wakati mwingine yanagumisha malezi na makuzi ya watoto, kiasi cha kuwafanya kukosa amani, utulivu na furaha. Watoto wasilishwe sumu ya kuchukia imani.

Mwishoni mwa mazungumzo kati ya wakuu wa Mashirika ya Kitawa na Kazi za Kitume, Baba Mtakatifu alitangaza kwamba, Mwaka 2015 utakuwa ni Mwaka wa Watawa; dhana inayoanza kufanyiwa kazi kwa sasa. Baba Mtakatifu anaendelea kuyashukuru Mashirika ya Kitawa na Kazi za Kitume kwa mchango wao katika maisha na utume wa Kanisa.

Mazungumzo haya yamehaririwa na
Padre Richard A. Mjigwa, C.PP. S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.








All the contents on this site are copyrighted ©.