2014-03-07 08:31:51

Mshikamano wa Kanisa na wagonjwa wa Ukimwi nchini Tanzania


Askofu mkuu Zygmunt Zimowski, Rais wa Baraza la Kipapa la shughuli za kichungaji kwa ajili ya wafanyakazi katika sekta ya afya, hivi karibuni, alizindua mradi wa kupima na tiba kwa wagonjwa wa Ukimwi, Jimbo Katoliki Shinyanga, Tanzania. Ni mradi unaoendeshwa kati ya Mfuko wa Msamaria mwema, Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania pamoja na Kampuni ya dawa kutoka Marekani ijulikanayo kama Gilead Sciences. RealAudioMP3

Zaidi ya watu 120, 000 wanatarajiwa kufaidika na mradi huu inayojikita katika: sheria na kanuni za tiba; maadili na utu wema. Watoto yatima watapewa kipaumbele cha pekee. Mradi huu ni kielelezo cha mshikakano wa dhati katika mchakato wa kumhudumia mtu mzima: kiroho na kimwili unaofanywa na Makanisa mahalia kama sehemu ya Uinjilishaji wa kina. Baraza la Kipapa la huduma za kichungaji kwa ajili ya wafanyakazi katika sekta ya afya linapenda kuunga mkono juhudi zinazofanywa na Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania katika Jimbo Katoliki la Shinyanga.

Hizi ni juhudi zilizofanywa kwa ushirikiano mkubwa kati ya Marehemu Askofu Aloysius Balina wa Jimbo Katoliki Shinyanga pamoja na Monsinyo Jean Marie Mupendawatu, Katibu mkuu wa Baraza la Kipapa la shughuli za kichungaji kwa ajili ya wafanyakazi katika sekta ya afya, ambaye mara kadhaa alitembelea Tanzania ili kuangalia uwezekano wa utekelezaji wa mradi huu kwa ajili ya kuwasaidia wagonjwa wa Ukimwi nchini Tanzania.

Askofu mkuu Zygmunt Zimowski anasema, Baraza la Kipapa linaendelea kushirikiana na kushikamana na Kanisa Barani Afrika katika huduma kwa wagonjwa kwa kutoa msaada wa hali na mali kadiri ya nafasi na uwezo uliopo. Kati ya miradi hii ni ule wa “Africae Munus” Dhamana ya Afrika, unaovijumuisha vyuo vikuu saba vya Kikatoliki Barani Afrika kwa lengo la kujenga mtandao wa majiundo makini kwa wafanyakazi katika sekta ya afya, Kusini mwa Jangwa la Sahara.

Baba Mtakatifu Francisko anaendelea kulikumbusha Kanisa kwamba, hata wagonjwa katika shida na mahangaiko yao, bado ni sehemu muhimu sana ya Fumbo la Mwili wa Kristo, yaani Kanisa. Wanapaswa kuheshimiwa, kuthaminiwa na kusaidiwa katika mahangaiko yao: kiroho na kimwili. Kumbe, Vatican itaendelea kushirikiana na Makanisa mahalia katika huduma za kiroho na kimwili kwa wagonjwa Barani Afrika.

Kati ya mambo yanayoendelea kupewa kipaumbele cha kwanza kwa wakati huu na Baraza la Kipapa la huduma za kichungaji kwa wafanyakazi katika sekta ya afya ni maandalizi kwa ajili ya ushiriki wa wagonjwa kwenye Ibada ya Misa Takatifu kwa ajili ya kumtangaza Mwenyeheri Yohane Paulo II kuwa Mtakatifu hapo tarehe 27 Aprili 2014.

Huu ni mwanga wa imani na matumaini yanayobubujika kutoka kwenye utakatifu na ushuhuda wa maisha ya Mwenyeheri Yohane Paulo wa Pili; ni kiongozi ambaye hakuficha kuonesha ugonjwa wake, akakubali kuubeba Msalaba wa maisha na utume wake kwa imani na matumaini, hadi siku ile alipoyamimina maisha na kujikabidhisha kwa Mwenyezi Mungu, mwingi wa huruma na mapendo kwa waja wake.








All the contents on this site are copyrighted ©.