2014-03-06 07:46:26

Ushiriki wa AMECEA katika mkutano mkuu wa SIGNIS mjini Roma


Mkutano mkuu wa Shirikisho la Wanahabari Wakatoliki kutoka sehemu mbali mbali za dunia limehitimishwa hivi karibuni mjini Roma. Huu ni mkutano unaofanyika kila baada ya miaka minne. Mwaka 2013 mkutano huu ulikuwa umepangwa kufanyika mjini Beirut, Lebanon, lakini haikuwezekana kutokana na sababu za kiusalama huko Mashariki ya Kati na matokeo yake umeadhimishwa mjini Roma kuanzia tarehe 25 Februari hadi tarehe Mosi, Machi 2014. RealAudioMP3

Katika mahojiano maalum na Radio Vatican Padre Chrisantus Ndaga, Katibu wa Idara ya Mwasiliano, Shirikisho la Mabaraza ya Maaskofu Katoliki Afrika Mashariki na Kati, AMECEA anasema, mkutano huu ulikuwa umegawanyika katika sehemu kuu mbili: Sehemu ya kwanza ilikuwa ni warsha kuhusu vyombo vya habari na sehemu ya pili ilijikita zaidi katika mikutano na chaguzi za kikanda. AMECEA kimsingi si mwanachama wa SIGNIS bali inasaidia kuratibisha mawasiliano kati ya SIGNIS na nchi waachama wa SIGNIS, Afrika Mashariki na Kati.

Padre Ndaga anasema, Nchi za AMECEA katika mkutano mkuu wa SIGNIS zilikuwa na uwakilishi mzito, uliosaidia pia kupata wajumbe wawakilishi wa nchi za AMECEA katika vikao vya SIGNIS. Huu ni mkutano ambao umeangalia mwelekeo wa tasnia ya habari kwa siku za usoni; mambo yanayoibuliwa na tamaduni mpya ya utandawazi na maendeleo ya sayansi na teknolojia pamoja na changamoto zinazoendelea kujitokeza kwa vijana wa kizazi kipya.







All the contents on this site are copyrighted ©.