2014-03-06 09:11:28

Maadhimisho ya Jumatano ya Majivu: Rarueni mioyo na si mavazi..


Jumatano kwa ajili ya Maadhimisho ya Jumatano ya Majivu, mwanzo wa kipindi cha siku arobaini za Kwaresima , Baba Mtakatifu Francisko , aliongoza Ibada ya Majivu na Misa , katika Kanisa la Mtakatifu Sabina la Aventino la hapa Roma.
Katika mahubiri yake , Papa alitoa mwaliko wa kumrudia Mungu, kwa sababu leo hii ndani ya jamii na Kanisa, mambo hayaendi sawa. Papa alionya, tunahitajika kutubu na kuongoka, maana tunaishi katika dunia bandia zaidi na zaidi. Bila kutambua hilo, tunamtenga Mungu kutoka upeo wa macho yetu. Kwaresima hivyo, unakuwa ni wakati wa kuamka na kutoka katika hali hiyo ya kuwa waovu siku hadi siku, na kuanza kuwa watu wema . Papa kabla ya Ibada ya Misa aliongoza Maandamano ya toba, kutoka Kanisa la Mtakatifu Anselm la Aventine.
ahubiri ya Papa yalizungumzia zaidi mambo matatu Mkristu anayotakiwa kuyafanya wakati huu wa kwaresima kuwa ni sala, kufunga na kutoa sadaka.
" Rarueni mioyo yenu na wala si mavazi yenu " ( Joel 2:13).
Kwa maneno hayo ya nabii Joel ,yaliyokuwa utangulizi wa liturujia , Papa alisema, yanaonyesha tabia ya uongofu wa moyo, wakati huu wa neema. Ni wito wa kinabii unatoa changamoto kwetu sote , bila ubaguzi, wenye kutukumbusha kuwa uongofu wa kweli si mabadiliko tu ya kuonekana kwa nje au kuwa mtu wa kutoleweka eleweka, lakini hasa ni kuwa na mageuzi ya moja kwa moja na kamili, kidhamiri na katika kutenda. Na hivyo Nabii Joel anatoa mwaliko kwetu sote wakati huu, tunapoianza safari ndefu na ngumu , ni wakati wa kufungua macho yetu na masikio, lakini hasa moyo , kuzamisha zaidi mtima ndani ya Neno la Mungu.
papa aliendelea kufafanua maana ya kujifunua kwa Mungu na kwa wengine akisema, wakati huu tunapoishi katika dunia inayozidi kuwa ya bandia, katika utamaduni wa kutenda bila ya kujali uwepo wa Mungu, Utamaduni unaopenda kumtenga Mungu kutoka upeo wa macho yetu, Kwaresima, inatoa wito kwetu sote, kustuka na kuamka , kukumbuka kwamba sisi ni viumbe tu, tulioumbwa na Mungu.
Papa alieleza na kuonya dhidi ya kujifungia wengine nje, pia hatari za kuyasahau matatizo na mateso ya watu wengine , kuwa ni changamoto kwetu , wakati wa kuanza safari yetu ya kubadilika katika kipindi hiki. Kipindi hiki kina ratiba kutembea pamoja na msalaba na sadaka.
Na kwamba, Injili ya ( Mt 6,1-6.16-18 ) inaonyesha vipengere muhimu katika safari hii ya kiroho kuwa ni sala, mafungo na sadaka. Vyote vitatu, havina haja ya kujionyesha kwa nje , wala kuonekana kwake kwa nje kutoa maana au thamani ya maisha kutegemea na wengine wanasema nini , au juu ya mafanikio lakini hasa ni jinsi gani tulivyo kwa ndani.
Papa aliyataja maombi kuwa ni nguvu ya Kikristo na kwa kila mtu anaye amini. Katika unyonge na udhaifu wa maisha yetu , tunaweza kumgeukia Mungu na kuwa na ujasiri kuwa wana wa Mungu na kuingia katika ushirika pamoja naye. Katika uso wa majeraha mengi yanayotuumiza na kuufanya moyo kuwa mgumu , tunahimizwa kupiga mbizi katika bahari ya maombi ambayo ni bahari ya upendo wa Mungu, ulio mkubwa kupita kiasi, kufurahia huruma yake. Kwaresima ni wakati wa sala, sala na ibada iliyo makini zaidi ambamo unakuwa ni wakati wa kuwa wakarimu zaidi kwa watu wahitaji waliopungukiwa , ni wakati wa kuwaombea mbele ya Mungu, wanao ishi katika hali nyingi ya umaskini na mateso.








All the contents on this site are copyrighted ©.