Ujumbe wa Kwaresima kwa Mwaka 2014 kutoka Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican inakuletea ujumbe wa Kwaresima kwa Mwaka 2014
kutoka Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania unaoongozwa na kauli mbiu "Ukweli utawaweka
huru. Yn. 8:32". Maaskofu wanazungumzia kuhusu umuhimu wa wongofu wa kweli unaomweka
mwamini huru; wajibu wa kuuishi, kuulinda na kuusimamia ukweli kishuhuda mintarafu
hali halisi ya Tanzania.
UTANGULIZI
Wapendwa Taifa la Mungu,
“Ukweli
utawaweka huru”. Safari ya maisha ya mwanadamu ni safari ya kutafuta uhuru, uhuru
ambao unamfungua mtu kutoka katika minyororo inayomfunga na kumfanya kuwa mhudumu
wa mazingira na hali yake. Chimbuko la uhuru wa kweli ni Mungu mwenyewe katika mpango
wake wa milele na huruma yake ya milele. Mungu ndiye asili na chanzo cha uhuru wa
kweli na tunafanywa kuwa huru kweli pale tunapoamua kwa dhati kuupokea ukweli utokao
kwa Mungu. Mungu ndiye ukweli wenyewe: “Ukweli wowote, bila kujali anayeusema, unatoka
kwa Roho Mtakatifu”, na popote tunapoukuta ukweli huo ni mali ya Mungu.
Wapendwa
Taifa la Mungu, tunapoanza safari ya Kwaresima ya mwaka huu, sisi Maaskofu wenu, tungependa
kuwakumbusheni ninyi na watu wote wenye mapenzi mema juu ya umuhimu wa kuishi katika
ukweli. Kuuishi ukweli na kuishi maisha yaliyojengwa juu ya msingi wa ukweli ni kushiriki
hasa maisha ya Mungu. Kama tunataka kujenga jamii yenye utu, haki, amani, upendo na
mshikamano wa kweli, ni lazima tuanze kwanza kujenga dhamiri zinazothamini na kuuenzi
ukweli. Pasipo ukweli jamii itasambaratika kwa sababu itakuwa imejengwa bila msingi.
Wapendwa Taifa la Mungu, Ukweli utawapeni uhuru kwa kuwa toka kuumbwa
kwa ulimwengu, Mungu aliye ukweli wenyewe alipanga na kunuia kwamba mwanadamu aliyemuumba
kwa sura na mfano wake, aishi katika uhuru kamili akimiliki na kuutiisha ulimwengu
wote (Mwa 1:28 ). Ni katika ukweli tunamjua, tunampenda na kumtumikia Mungu. Ni
katika ukweli tunadhihirisha kuwa tumeitwa kuwa wana huru katika ufalme wa Baba wa
milele.
Ukweli na uhuru ni dhana zinazoenda pamoja. Penye ukweli pana uhuru
na penye uhuru pana ukweli. Kama vile mtu huru awezavyo kuuishi ukweli kwa kuwa uhuru
wake humfanya ajitegemee kifikra, kimaamuzi na kiutendaji ndivyo pia jamii ya watu
na hata taifa huru liwezavyo kujitegemea kifikra, kimaamuzi na kiutendaji.
Kwa
maisha, kifo na ufufuko wa Kristo, waamini wamewekwa huru na wanaitwa kuutafuta na
kuusimamia ukweli. Waamini wanaalikwa kuutafuta, kuujua na kuulinda ukweli katika
nyanja zote za maisha.
SURA YA KWANZA WONGOFU WA KWELI HUTUWEKA HURU
Mungu
alipenda kujifunua kwa wanadamu kupitia manabii na mwanawe wa pekee Bwana wetu Yesu
Kristo. Hata leo, Roho Mtakatifu analiongoza Kanisa katika kuendelea kuujua ukweli
wa kiimani katika safari ya pamoja ya kiroho kuelekea uhuru kamili wa roho zetu.
Ukweli wa kiimani huleta uhuru wa kiroho. Mwaka uliopita Kanisa liliadhimisha Mwaka
wa Imani ikiwa ni sehemu ya kuwakumbusha wanakanisa wote juu ya wajibu wao wa kiimani
katika Kanisa na katika jamii.
Kwa kuishi ipasavyo imani yetu ya kikristo
tunashiriki wajibu wa kuujenga Ufalme wa Mungu ambao mojawapo ya nguzo zake saba za
msingi ni ukweli! Hakika, ufalme wa Mungu, kama Mama Kanisa anavyotangaza katika utangulizi
wa Misa ya sherehe ya Kristo Mfalme ni ufalme wa UZIMA na KWELI, ufalme wa NEEMA na
UTAKATIFU, ufalme wa HAKI, MAPENDO na AMANI. Mungu wetu ni UKWELI na ni MKWELI. Tunasadiki
na kukiri kwamba hadaganyi wala hadanganyiki. Imani ni wajibu wa kushiriki kuujenga
Ufalme wa Mungu, ufalme ambao msingi wake ni ukweli, kwa sababu Mungu ni ukweli.
Mwanadamu
aliyekombolewa kwa damu ya thamani kubwa sana ya Kristo iliyomwagika pale Kalvari,
amepata kurudishiwa hadhi ya kuwa mwana huru wa Mungu akikombolewa kutoka utumwa wa
dhambi. Uhuru anaoupata mwanadamu una gharama kubwa na thamani kubwa. Uhuru wa kweli
ni uhuru ndani ya Mungu; ni uhuru katika Mungu. Uhuru wa kweli huambatana na utii
wa sheria ya Mungu na uwajibikaji unaodai unyenyekevu na nidhamu ya hali ya juu. Uhuru
huu ni kinyume na uhuru usio na mipaka ambao jamii ya sasa inadai,uhuru ambao hupingana
na malengo ya Muumba na taratibu na miongozo halali mbele za Mungu iliyowekwa na jamii. Kanisa,
ukweli na uhuru
Kanisa ambalo ni ishara ya wokovu na alama ya uwepo hai wa
Kristo aliye njia, ukweli na uzima katika ulimwengu wa sasa ni sisi tulioalikwa kuwa
Familia ya Mungu. Kwa kumkiri Kristo na kwa kubatizwa kwetu tumekuwa Rafiki na wadau
wake Yesu Kristo (Yn 15: 14). Kwa namna hiyo sisi sote Familia ya Mungu – Wakleri,
Watawa na Waumini Walei – tu chombo mikononi mwa Kristo kwa kushiriki kikamilifu kazi
ya Kristo ya kuwakomboa watu.
Kwa mantiki hiyo, Kanisa linao wajibu wa kwanza
kabisa kuulinda ukweli, kuusimamia, kuushi na kuutangaza. Kanisa ni chombo kiletacho
wokovu kwa ulimwengu na kuwaweka huru wanadamu walio katika utumwa unaojidhihirisha
katika sura mbalimbali kama vile, umasikini, ufisadi, rushwa, ushirikina, magonjwa,
siasa chafu, kutokuwajibika, ubinafsi,nk.
Kanisa ni chombo cha Kristo cha kuwaletea
watu uhuru wa kweli. Roho wa Bwana, aliye juu ya Yesu (Lk 4:18,19) yuko pia juu ya
Kanisa lake ambalo analituma kuwafungulia watu vifungo vyao mbalimbali na kuwaachia
huru waliosetwa (Lk 4:18-19).
Ukweli kama tunu ya kimungu lazima uote mizizi
katika mioyo ya wanadamu walioumbwa kwa sura na mfano wake (Kut 1:26). Ni wajibu wa
kila mwanadamu kuutafuta ukweli na kuujua. Kwa njia ya ufahamu, mwanadamu anaalikwa
kuutafuta ukweli kwani ndio njia pekee ya kumweka huru na kuufikia wokovu. Maana Mungu
amemwachia mwanadamu uhuru kusudi aifuate nia yake (YBS 14:15), na hivyo amtafute
Muumba wake kwa hiari, na hatimaye aufikie ukamilifu ulio bora na wenye heri, pasipo
shuruti na kwa kuambatana na Mungu. Kanisa linamsaidia mwandamu kufanikisha kuufikia
ukweli na kwa uhuru kupitia neema za Mungu.
SURA YA PILI WAJIBU
WA KUUISHI, KUULINDA NA KUUSIMAMIA UKWELI KISHUHUDA
Waamini waliowekwa huru
na Kristo, wanao wajibu wa kuujua ukweli, kuutafuta, kuulinda na kuusimamia kwa lengo
la kuleta huru wa kweli kwa manufaa ya wote. Huko ndiko kuwa mfuasi wa Kristo aliyesema:
“Mimi nilikuja ulimwenguni; ili niishuhudie kweli. Kila aliye wa hiyo kweli hunisikia
sauti yangu” (Yn 18:38).
Jamii leo hii imegawanyika juu ya uhuru ambao wanajamii
wanapaswa kuwa nao. Wazazi wanaamini kuwa uhuru ni kutenda jambo lolote bila kubughudhiwa
na yeyote, hata kama tendo hilo ni kinyume na misingi ya maadili. Watoto wanataka
uhuru binafsi katika kupanga na kuamua mambo yanayowahusu. Watoto wasingependa kupokea
malezi na maelekezo iwe ni ya wazazi au ya jamii. Vijana wanapenda kuamua mambo yao
kama wanavyoona, wakipuuzia uzoefu na ushauri wa wakubwa wao. Tujiulize: Je, huu ndiyo
uhuru tuutafutao? Katika mazingira kama haya kinachotafutwa si uhuru bali kuishi kwa
kuheshimu vionjo binafsi. Ni muhimu sana kwa wanafamilia kuwa na uhuru wa pamoja katika
kupanga na kuamua masuala kifamilia.
Tukijiruhusu kama wanajamii kuishi katika
uholela upendo unatoweka. “Usikubali kitu chochote kuwa ni ukweli kama kinakosa upendo.
Na usikubali kitu chochote kuwa ni upendo kama kinakosa ukweli! Hali moja bila nyingine
ni uongo unaoharibu”. Kwa sababu “ni katika ukweli tu ndipo upendo inang’aa, ni katika
ukweli tu ndipo tunapoweza kuuishi upendo kwa hakika”. SURA YA TATU HALI HALISI
YA TAIFA LETU
Taifa lenye umri wa miaka 50 ya uhuru ni taifa lililokwishavuka
uchanga. Ni taifa kijana lililo katika umri wa kujenga juu ya misingi iliyowekwa
kwa manufaa ya wote. Ni taifa linalojitegemea. Bila msingi huo, mengine yote, hata
kama yanaonekana yanang’aa yatakuwa yanasaliti mustakabali wa kweli wa taifa letu.
Tusijidanganye. Bila msingi wa kujitegemea na kutafuta manufaa ya wote (common good)
taifa hili litaanguka. Kama halianguki leo, kesho ni lazima litaanguka. Tunajiuliza,
uko wapi ujasiri wa Taifa letu? Imepotelea wapi fahari ya kujitawala, si kisiasa tu,
bali kiuchumi, kifikira na kijamii? Imepotelea wapi ile mbegu ya uzalendo iliyopandwa
na waasisi wa taifa letu? Imeishia wapi heshima ya kuthamini utu, kuheshimu imani
ya asiyeamini kile nisichokiamini na kutafuta ufumbuzi halisi wa matatizo yanayotukabili?
Tumepoteza
dira ya kujitegemea kimaamuzi na kimkakati. Tumefikia mahali pa kuamini kwamba maendeleo
yataletwa kwa kaulimbiu zinazobadilika badilika kila siku. Katika mazingira ya sasa,
watu wachache, kwa sababu binafsi na kwa manufaa binafsi wanapotosha ukweli na kutafuta
njia za kulinda maslahi yao kwa kutumia mifumo isiyokubalika, lakini inayosimikwa
na kuhalalishwa ili kulinda maslahi binafsi. Hali hii inajidhihirisha kupitia matumizi
mabaya ya madaraka, mikataba mibovu, kupindisha sheria, kufumbia macho uhalifu, nk.
Uhuru wa kweli haujengeki katika misingi dhaifu ya ubinafsi na haulengi kumfanya mtu
yeyote yule awe juu ya sheria za haki na taratibu za uadilifu. Na kimsingi, hakuna
maendeleo ya kweli kama watu hawaheshimu haki ya msingi ya kuujua ukweli na kuishi
kadiri ya ukweli huo.
Katika mazingira kama haya Kanisa haliwezi kukaa pembeni
na kutazama tu kwa sababu nalo lina wajibu wa kuijenga jamii. Kanisa lina wajibu wa
kuangalia, kuboresha na kuikosoa mienendo ya kijamii na kisiasa inayohatarisha ustawi
wa jamii nzima na hivyo kuathiri kazi ya Kristo ya kumkomboa mwanadamu na kuusimika
Ufalme wa Mungu; ufalme unaojidhihirisha katika kutamalaki kwa ukweli, haki na amani.
Kanisa litaendelea kusisitiza ukweli huu kwamba; “Ili kuunda maisha ya kisiasa yaliyo
kweli ya kibinadamu, hakuna lililo bora zaidi kuliko kustawisha ndani ya watu hisia
za haki, upendo na huduma kwa manufaa ya wote”. Hapa tungependa kuelezea mambo machache
yanayoivuruga nchi yetu. Uvunjifu wa amani
Taifa letu linazidi kupoteza
tunu bora ya amani ambayo waasisi wa taifa letu wametuachia. Katika siku za karibuni
yamekuwepo matukio ya mauaji, watu kumwagiwa tindikali kwa sababu ya imani yao au
visasi na hata mauaji kwa kutumia mabomu. Uhasama wa kidini na matukio ya kijasusi
na ugaidi dhidi ya raia yanaonekana kushamiri. Kumekuwapo na matumizi makubwa ya nguvu
upande wa vyombo vya dola vikitumia silaha za moto na za kivita. Wimbi la wananchi
kutotii sheria na taratibu za nchi linakua. Tunakwenda wapi?
Amani lazima ilindwe
ndani na nje ya mipaka ya nchi yetu. Hata hivyo, amani sio tunu inayojitegemea peke
yake kwa kuwa amani ya kweli inazaliwa ndani ya mioyo yenye kujali misingi ya utu,
haki, heshima, ukweli na umoja. Fikra tofauti na hizo, huzaa mioyo potofu, na mioyo
potofu haiwezi kutoa amani. Rushwa na madawa ya kulevya
Mapambano dhidi
ya rushwa na madawa ya kulevya yamegeuka kuwa wimbo unaochosha kwa sababu hakuna dhamira
ya dhati ya kuitokomeza. Uongozi wa juu unapotamka hadharani kuwafahamu watoa rushwa,
wapokea rushwa na wafanyabiashara wa madawa ya kulevya lakini hakuna hatua zozote
zinazochukuliwa ni hali inayotisha sana. Wakati umefika ambapo lazima tuwe wakweli
kuhusu mapambano dhidi ya rushwa na madawa ya kulevya. Hatuwezi kuwa huru kuhusu rushwa
na madawa ya kulevya kama hatujawa wakweli kuhusu mapambano dhidi ya rushwa na madawa
ya kulevya. Wanaopiga vita rushwa majukwaani, ndio wanaoomba na kupokea nje ya jukwaa.
Isitoshe rushwa ndiyo ngazi waliyoitumia na wanayoitumia kufika jukwaani. Katika mazingira
kama haya hatujengi Taifa bali tunalibomoa na historia itatuhukumu. Hatuna budi kuunda
misingi imara ya utawala bora. Tukumbuke daima kuwa utawala bora bila uwajibikaji
na kuwajibishana ni kiini macho. Kukua kwa matabaka katika jamii
Tofauti
kubwa sana za kiuchumi zinazidi kupanua utengano wa kimatabaka kati ya wenye nguvu
za kiuchumi na wasio na kitu. Wenye nguvu kiuchumi sasa wanamiliki uchumi, wanamiliki
siasa na hatima ya fukara, na kwa fedha wananunua haki ya wanyonge.
Mgawanyo
mbovu wa rasilimali za nchi unatisha. Ardhi inamilikiwa na wachache kwa kivuli cha
uwekezaji mkubwa huku wananchi wakiahidiwa ajira kwa kuwa vibarua kwenye mashamba
hayo badala ya kuwezeshwa kumiliki ardhi na kuitumia kwa faida. Haya ni masuala yanayomtia
hofu mtu yeyote anayejali na kuthamini mustakabali wa taifa letu. Siasa kuingilia
weledi
Tatizo la siasa kutawala mifumo ya ujenzi wa misingi ya maendeleo linakua
kwa kiwango cha kutia hofu. Kwa mfano, siasa na wanasiasa wanaathiri mfumo wa utoaji
wa elimu nchini kiasi cha kulifanya taifa hili kuwa kama taifa lisilojali mustakabali
wake. Yamekuwepo maneno mengi na mipango ya zimamoto isiyofanyiwa utafiti wa kina
na utendaji umekuwa hafifu sana. Uthabiti katika kusimamia utekelezaji wa mipango
ya maendeleo hauonekani na badala yake porojo zimetawala. Imejitokeza hali ya wale
waliopewa dhamana ya kusimamia masuala ya elimu kwa mfano kukosa unyenyekevu wa kuwasikiliza
na kushauriana na wataalamu katika nyanja hizi. Kila mara zinaibuka sera ambazo msingi
wake ni ubunifu usiozingatia weledi na hivi kuifanya elimu kudidimia. Mchakato
wa Katiba mpya
Katiba kama moyo wa taifa ni chombo kinachopaswa kutengeneza
misingi ya mfumo wa maisha mazima na uhai wa Taifa letu. Ukweli wote na uhuru wote
wa Taifa unabebwa na Katiba. Iwapo mchakato wa katiba mpya hautaendeshwa kwa ukweli
na uhuru, hatutaweza kupata katiba yenye kubeba ukweli na uhuru wote kuhusu taifa
letu. Tunarudia tena kutamka kuwa zoezi hili adhimu na la muhimu kwa mustakabali wa
Taifa limeharakishwa mno. Sasa tunaona zoezi zima limehodhiwa na wanasiasa. Mchakato
wa katiba mpya unadai kuwepo kwa fadhila ya kijamii ya kutafuta manufaa ya wote (common
good). Katiba si mali ya wanasiasa bali ni mali ya wananchi. Tunapenda kuialika jamii
yote kuitendea haki nchi yetu. Tukae chini na tuzipime kila hatua zetu katika zoezi
hili na tuone kama zinakidhi kipimo cha «Hekima, Umoja na Amani». Hekima ituongoze
kulinda umoja wa Taifa letu na utuepushe na kishawishi cha kubaguana na kutengana.
Kwa kuzingatia hilo umoja huo utatuongoza katika njia ya amani.
Uharibifu wa
mazingira
Tishio kubwa la kimaangamizi kwa vizazi vijavyo linatokana na ukweli
kuwa kumekuwepo na uharibifu mkubwa wa mazingira. Maendeleo yanagharama yake. Kiu
ya kweli ya maendeleo ni lazima iambatane na ulazima wa kuwa makini katika kutunza
mazingira na uthabiti wa uumbaji. Vyanzo vya maji na kingo za mito zimeharibiwa kwa
kuruhusu shughuli za kilimo kufanyikia maeneo hayo, kwa kuruhusu makazi ya watu, viwanda
kujengwa na kuruhusu takataka ya sumu kutoka viwandani na migodini kutiririkia kwenye
vyanzo vya maji, nk. Ukataji wa miti umeshamiri na baadhi ya misitu ya asili imepotea.
Kwa sababu hiyo tumechangia sana katika kusababisha mabadiliko ya tabia nchi ambayo
athari zake sasa zinajionesha waziwazi. Ukame, njaa, mafarakano kati ya wakulima na
wafugaji na kuenea kwa jangwa ni vitisho vilivyo dhahiri mbele yetu. Huu ni ukweli
kuwa tumeshindwa kuzingatia agizo la Mungu la kuitawala na dunia kuutiisha ulimwengu.
Tunahitaji sasa kubadilika ili ukweli utawale, tupate uhuru kamili kwa kuwajibika
kuyalinda na kuyatunza mazingira kwa faida ya kizazi cha sasa na vizazi vijavyo.
Ni wajibu wetu Waamini Wakatoliki kuulinda ukweli na kuusimamia kiushuhuda. Jitahada
za namna hii zina gharama yake kwa kuwa zinahitaji ujasiri wa kinabii na utayari wa
kuteseka na hata ikibidi kutoa sadaka kubwa ya uhai. HITIMISHO
Wapendwa
Taifa la Mungu, tunapenda kuwahimiza kwa maneno haya tukisema: “Inunue kweli, wala
usiiuze. Naam, hekima na mafundisho na ufahamu” (Mith 23:23). Ukweli ni msingi wa
lazima na unapaswa kuwa wa kudumu kwa tendo lolote ili liweze kuitwa kuwa ni adilifu.
Ukweli unapaswa kuzijenga dhamiri zetu ili kumsaidia mwanadamu kupata mwanga unaofukuza
mikanganyiko.
Katika ulimwengu usiojali ukweli, uhuru unapoteza msingi
wake na mwanadamu anakuwa mhanga wa vurugu ya vionjo na kutawaliwa kwa hila, iliyojidhihirisha
waziwazi au iliyojificha. Hivi ni mwaliko kwetu sote “tuishike kweli katika upendo
na kukua hata tumfikie yeye katika yote, yeye aliye kichwa, Kristo” (Efe 4:15). Kwa
sababu upendo “haufurahii udhalimu, bali hufurahi pamoja na kweli” (1Kor 13:6).
Ni
sisi Maaskofu wenu,
Mhashamu Askofu Tarcisius Ngalalekumtwa, Rais wa Baraza
la Maaskofu Katoliki Tanzania, Iringa Mwadhama Polycarp Kardinali Pengo, Dar es
Salaam Mhashamu Askofu Mkuu Josaphat Lebulu, Arusha Mhashamu Askofu Mkuu Paul
Ruzoka, Tabora Mhashamu Askofu Mkuu Yuda Thaddaeus Ruwa’ichi, Ofm Cap, Mwanza, Mhashamu
Askofu Telesphor Mkude, Morogoro Mhashamu Askofu Gabriel Mmole, Mtwara