2014-03-04 08:36:57

Waziri wa ulinzi Filipe Nyusi kupeperusha bendera ya FRELIMO wakati wa uchaguzi mkuu nchini Msumbiji


Chama cha Tawala cha FRELIMO nchini Msumbiji kimemteua Bwana Filipe Nyussi, Waziri wa Ulinzi kupeperusha bendera ya chama hiki wakati wa kinyang'anyiro cha uchaguzi mkuu nchini Msumbiji, unaotarajiwa kufanyika mwezi Oktoba, 2014. Kama mambo yote yakienda sawa, basi Bwana Filipe Nyussi anatarajiwa kurithi kigoda cha Rais Armando Emilio Guebuza.

Uamuzi huu umetolewa na Kamati kuu ya Chama cha FRELIMO katika kikao chake kilichohitimishwa hivi karibuni. Katika kinyang'anyiro hiki, Bwana Filipe Nyussi alikuwa anachuana na Waziri mkuu mstaafu Luisa Diogo ambaye kadiri ya duru za kisiasa zinaonesha kwamba, alikuwa anaungwa mkono na kambi ya Rais mstaafu Joakim Chisano wa Msumbiji.

Chama cha FRELIMO kimekuwa kikishinda uchaguzi mkuu tangu mwaka 1992. Bwana Filipe Nyussi anatarajiwa kupambana na nguri za upinzani: Alfonso Dhlakama kutoka Chama RENAMO pamoja na Davis Simango kutoka Chama cha MDM.







All the contents on this site are copyrighted ©.