2014-03-04 08:21:48

Wasikilizeni wanawake kwa makini!


Kardinali Walter Kasper ambaye hivi karibuni alipewa dhamana na Baraza la Makardinali kuwamegea kuhusu uzuri wa ndoa na changamoto zake katika ulimwengu mamboleo katika mahojiano maalum na Gazeti la "Avvenire" linalomilikiwa na Baraza la Maaskofu Katoliki Italia anasema kwamba, kuna haja kwa Mama Kanisa kutambua na kuthamini wito, utume na dhamana ya wanawake ndani ya Kanisa.

Ni matumaini ya Kardinali Kasper kwamba, mchakato wa Maadhimisho ya Sinodi za Maaskofu kuhusu Familia zitakazofanyika Mwaka 2014 na Mwaka 2015 zitatoa mwanya wa kuwasikiliza wanawake. Hii inatokana na ukweli kwamba, bila mwanamke, Familia iko mashakani. Huu ni ujumbe mzito wakati huu Mama Kanisa anapoendelea kuhimiza umuhimu wa kukuza na kuimarisha tunu msingi za maisha ya ndoa na familia.

Kimsingi wanawake hawajasikilizwa kwa makini ndani ya Kanisa. Umefika wakati anasema Kardinali Kasper kuwasikiliza na kuwashirikisha katika maisha na utume wa Kanisa katika ngazi mbali mbali na hasa zaidi katika vikao vyenye kutoa: sera, mikakati na maamuzi. Kanisa bila utume na ushiriki mkamilifu wa wanawake, linaweza kukosa dira na mwelekeo sahihi.

Sifa na wasifu wa kuwashirikisha wanawake katika maisha na utume wa Kanisa, ziwe ni sawa kama inavyotolewa kwa wanaume; yaani: weledi, uzoefu wa kazi, ari na moyo wa huduma kwa Kristo na Kanisa lake. Ushiriki wa wanawake anasema Kardinali Kasper unaweza kulisaidia Kanisa kuwa na mwono mpana zaidi katika mikakati yake ya kichungaji.

Kardinali Walter Kasper anawapongeza wanawake wanaoendelea kujitoa bila ya kujibakiza kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya Kanisa kwa kusimama kidete na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii. Hawa ndio Wamissionari wanaojisadaka katika huduma za elimu, afya na maendeleo ya Jamii hata wakati mwingine wanajikuta katika mazingira hatarishi. Kanisa linapaswa kuwatambua na kuwatia moyo ili kusonga mbele kwa imani na matumaini zaidi katika maisha na utume wa Kanisa.

Kardinali Kasper anasema, sauti ya wanawake inapaswa kusikilizwa kwenye vikao mbali mbali vya Kanisa vinavyotoa maamuzi kuhusu sera na mikakati ya maisha na utume wa Kanisa.







All the contents on this site are copyrighted ©.