2014-03-03 09:08:29

Kampeni ya Kwaresima, Baraza la Maaskofu Katoliki Kenya kwa Mwaka 2014


Maana mmejua neema ya Bwana wetu Yesu Kristo, jinsi alivyokuwa maskini kwa ajili yenu, ingawa alikuwa tajiri, ili kwamba ninyi mpate kuwa matajiri kwa umaskini wake. Ndiyo kauli mbiu inayoongoza ujumbe wa Baba Mtakatifu Francisko katika kipindi cha Kwaresma kwa Mwaka 2014, kinachoanza rasmi kwa Jumatano ya Majivu, tarehe 5 Machi 2014 hadi tarehe 17 Aprili 2014. RealAudioMP3
Hiki ni kipindi cha toba na wongofu wa ndani; kipindi cha kusali, kufunga na kutenda matendo ya huruma. Ni kipindi ambacho waamini wanaalikwa kwa namna ya pekee kufanya tafakari ya kina ya Neno la Mungu, ili kuweza kuimwilisha kama sehemu ya Imani tendaji!
Baraza la Maaskofu Katoliki Kenya katika Kampeni yake kwa Kipindi cha Kwaresima kwa Mwaka 2014 linawaalika waamini na watu wote wenye mapenzi mema kutafakari kwa kina kuhusu mafao ya wengi na tunu msingi za maisha ya ndoa na familia.
Akifafanua kuhusu Kampeni ya Kwaresima kwa mwaka huu, Askofu mkuu Zacchaeus Okoth, Mwenyekiti wa Tume ya haki na Amani, Baraza la Maaskofu Katoliki Kenya anasema, kwamba, Juma la kwanza, waamini wanaalikwa kutafakari na kujadiliana kuhusu matumizi bora na sahihi ya maliasili inayopatikana nchini Kenya kwa ajili ya mafao ya wengi.
Hii inatokana na ukweli kwamba, Kenya inaendelea kugundua utajiri mkubwa wa maliasili ambao unaweza kuwa ni baraka au balaa. Ikiwa kama wananchi wa Kenya wataungana kwa dhati wanaweza kuwashinikiza viongozi wa Serikali kuhakikisha kwamba, utajiri huu unatumika kwa ajili ya mafao ya wengi.
Baba Mtakatifu Francisko ameitisha Sinodi Maalum kwa ajili ya Maaskofu, itakayokuwa na dhamana ya kupembua na kuchambua changamoto za kichungaji zinazojitokeza katika maisha na utume wa familia. Baraza la Maaskofu Katoliki Kenya, katika Juma la Pili, wanawaalika waamini na watu wote wenye mapenzi mema kutafakari kuhusu. Familia na Imani. Taasisi ya familia kwa sasa inakabiliana na changamoto nyingi katika maisha na utume wake.
Askofu mkuu Okoth wa Jimbo kuu la Kisumu, Kenya anasema, hivi karibuni wananchi wa Kenya wameshuhudia baadhi ya wabunge wakijadili muswada wa sheria unaogusa na kutikisa misingi ya maisha ya ndoa na familia inayosigana kimsingi na tunu, mila na tamaduni njema za Kiafrika na Kikristo. Katika majadiliano na tafakari, waamini na watu wenye mapenzi mema wajadili kwa kina na mapana jinsi ya kupambana na tabia hizi zinazotaka kuhalalisha mmong’onyoko wa tunu msingi za kimaadili na utu wema zinazotaka kubomoa na kusambaratisha familia. Wananchi wanapaswa kuungana na kushikamana kwa pamoja ili kukabiliana na changamoto hizi katika maisha na utume wa ndoa na familia.
Katika kampeni ya Kipindi cha Kwaresima, Juma la tatu, waamini wanaalikwa kujikita zaidi katika tafakari inayolenga kujenga na kudumisha misingi ya umoja na mshikamano wa kitaifa pamoja na Amani, zawadi kutoka kwa Mungu lakini inamshirikisha na kumwajibisha binadamu. Wananchi wa Kenya wanahamasishwa kujenga na kuimarisha umoja wa kitaifa, kwa kung’oa uchoyo na ubinafsi; chuki na uhasama, ili kuimarisha umoja wa kitaifa. Ikumbukwe kwamba, Amani inashamiri pale ambapo haki imepewa kipaumbele cha kwanza.
Askofu mkuu Okoth anawaalika waamini katika Juma la nne kujikita zaidi katika tafakari inayopembua kuhusu utawala bora. Kuna kasoro nyingi zinazoendelea kujitokeza katika masuala ya uongozi ndani ya Serikali, Vyama vya Kisiasa pamoja na Taasisi mbali mbali nchini Kenya. Utawala bora ni kigezo msingi cha ustawi na maendeleo ya nchi. Utawala bora unapaswa kupata chimbuko lake ndani ya familia na katika Kanisa. Lengo ni kujikosoa ili kuimarisha nguvu ya kimaadili, ili kuweza kufuatilia masuala ya utawala bora kutoka kwa wengine!
Wananchi wanapaswa kushirikishwa kikamilifu katika kukuza na kuimarisha utawala bora; mada itakayojadiliwa kwa kina na mapana katika Juma la tano la Kipindi cha Kwaresima. Jamii inashuhudia kishawishi cha watu kutaka kujitajirisha wenyewe kwa kuhakikisha kwamba, wanatumia kila fursa inayopatikana kwa ajili ya mafao binafsi. Kanisa linawahamasisha waamini kushiriki kikamilifu katika mchakato wa uchaguzi, kwa kujielekeza zaidi katika uwajibikaji, ukweli na uwazi katika matumizi ya fedha na mali za Serikali.
Kwaresima ya Mwaka 2014 anasema Askofu mkuu Zacchaeus Okoth, Mwenyekiti wa Tume ya haki na Amaniya Baraza la Maaskofu Katoliki Kenya, kiwe ni kipindi kwa ajili ya kufunga na kusali ili kuiombea Kenya. Lengo ni kujenga na kuimarisha umoja na mshikamano wa kitaifa, kila mwananchi akiheshimiwa na kuthaminiwa utu wake.
Imehaririwa na
Padre Richard A. Mjigwa. C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.








All the contents on this site are copyrighted ©.